1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Real Madrid yaweka historia mjini Cardiff

Bruce Amani
4 Juni 2017

Mabao mawili ya Cristiano Ronaldo yaliisaidia Real Madrid kunyakua taji kubwa kabisa la kandanda barani Ulaya na kuweka historia ya kuwa timu ya kwanza kutetea Kombe la Ligi ya Mabingwa.

https://p.dw.com/p/2e6Rr
Juventus vs. Real Madrid - UEFA Champions League Final Pokal
Picha: Reuters/C. Recine Livepic

Mreno huyo alifunga bao la kwanza na tatu katika ushindi wao wa mabao manne kwa moja dhidi ya klabu ya Italia Juventus mjini Cardiff jana usiku. Mabao mengine ya Madrid yalifungwa na Casemiro na Marco Asensio wakati la Juventus lilifungwa na Mario Mandzukic. Lilikuwa kombe la 12 la Real Madrid.

Juventus walianza kwa kasi na kuutawala mchezo lakini wakashindwa kushinda Kombe hilo kwa mara ya tatu na badala yake wakapoteza fainali yao ya saba katika kile ambacho huenda kilikuwa ni nafasi ya mwisho kwa mlinda mlango nguli Gianluigi Buffon kushinda dimba hilo.

Safi inayosifika ya ulinzi ya Juve ilifungwa mabao mengi kaika fainali ya jana kuliko matatu waliyofungwa katika mecho 12 za awali katika dimba hilo, na mchezaji aliyeingia kama nguvu mpya Juan Cuadrado akapewa kadi nyekundu katika dakika za mwisho mwisho.

UEFA Champions League Final  - Juventus v Real Madrid  - Tor Mandzukic - 1:1
Mandzukic alisawazisha kwa njia ya ustadi mkubwaPicha: Getty Images/L. Griffiths

"Hakika leo ni siku ya kihistoria…najivunia sana kila mchezaji”, alisema kocha Zinedine Zidane.

Kiungo Toni Kroos alisema: "kushinda Champions League ni kitu kisichoaminika lakini kutetea kombe hilo ni kitu kitu cha kipekee”.

Ronaldo sasa ndiye mfungaji wa mabao mengi katika dimba hilo, ambapo amefunga 12 na kumpiku Lionel Messi wa Barcelona ambaye ana 11, na ni mchezaji wa pili baada ya nguli wa zamani wa Real Alfredo Di Stefano kufunga bao katika fainali tatu za Ulaya.

"Huu ni msimu mzuri sana,” alisema Ronaldo. "Nna furaha kuukamilisha kwa kushinda Champions League. Sote tuna furaha…”. Aliongeza CR7

Buffon alikiri "kusikitishwa sana, kwa sababu tulidhani tumefany akila tulwezalo ili kucheza fainali hii na kushinda. Kushinda kombe hili unapaswa kuwa na nguvu kuliko wengine wote. Walistahili kushinda."

Kocha wa Juve Maximiliano Allegri alisema "tulicheza vizuri katika kipindi cha kwanza lakini Real wakaongeza kasi katika kipindi cha pili nasi tukakwama”

Mwandishi: Bruce Amani/DPA
Mhariri: Sekione Kitojo