1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ripoti ya shirika la waandishi wasio na mipaka 2008

Soric, Miodrag13 Februari 2008

Shirika la waandishi wasio na mipaka limetoa leo ripoti yake 2008 leo ,juu ya hali ya waandishi habari mwaka jana 2007 .

https://p.dw.com/p/D71x

Waandishi habari 80 waliuwawa 2007 ,idadi kubwa kabisa katika muda wa miaka 13. Ripoti hiyo ya Shirika la waandishi wasio na mipaka linalojulikana kwa lugha ya kifaransa kama " Reporter Sans Frontieres" kwa mara nyengine tena limeziorodhesha nchi za kiafrika ambako waandishi habari wamekumbwa na hali ngumu na hata kuuwawa. Hizo ni Somalia, Zimbabwe, Niger na Tchad. Uhuru wa vyombo vya habari umeendelea kukandamizwa pia huko Korea kaskazini, Sri Lanka na pia katika mataifa ya Asia ya kati, Turkmenistan na Uzbekistan.
Ni watawala katika nchi hizo na nyengine nyingi ambao ndiyo wanaobeba dhamana ya hali hiyo ya kuwakandamiza raia wao wenyewe. Kama alivyoandika mwana falsafa wa kiingereza katika karne ya 19 John Stuart kuwa " taifa linalowakandamiza watu wake wadogo, lisishangae siku moja kuona kwamba hao wadogo wanashindwa kufanya lolote kubwa kwa sababu ya kukangamizwa huko."
Katika wakati huu wa utandawazi ukandamizaji katika nchi kadhaa ndiyo kwanza umezidi makali. Lakini mbali na sababu za kisiasa kuna pia sababu za kiuchumi katika ukandamizaji wa uhuru wa vyombo vya habari. Kufungwa midomo waandishi habari, hufungua milango ya rushwa , upendeleo, na urasimu. Mwisho yote huzoroteshwa na dola.
Ni jambo lisiloweza kuaminika kuona uhuru wa vyombo vya habari unakandamizwa katika awamu muhimu katika nchi fulani na hivyo kuzusha wasi wasi kwa usalama na maendeleo. Hii ndiyo hali inayokutikana mjini Mosko wakati Urusi ikielekea kwenye uchaguzi wa rais mwezi Machi. Maafisa wanataka lazima mgombea wa chama tawala ajinyakulie zaidi ya 70 asili mia ya kura. Ndiyo maana dola inadhibiti vituo vya redio na televisheni kumpigia debe Dimitri Medvedev achukuwe nafasi ya kiongozi wa taifa kama mrithi wa Vladimir Putin.
Ukweli ni kwamba Putin hataki mgombea wake ashindwe na anajua jinsi ya kuvidhibiti vyombo vya habari. Chini ya yote haya , hatimae Viongozi wa mataifa ya magharibi katika mkutano ujao wa kilele hawana budi kutuma ujumbe makhsusi kwa rais ajaye kwamba hii sio njia ya kidemokrasi ya kushika madaraka.
Bila shaka Urusi itasonga mbele kwa sababu ya utajiri wake wa mali asili na nguvu zake za kijeshi. Lakini wakati wa kuzingatia ni sasa na kama mtu anaheshimu utajiri mkubwa wa utamaduni wa nchi hiyo na wasomi wake, inafaa pia kuangalia jinsi waandishi habari werevu walioonyesha ujasiri wao mnamo miaka ya 90, sasa wanafanya kazi katika mazingira na kiwango gani. Urusi ni sehemu ya Ulaya na ni jukumu la ulaya kutupia jicho hatari inayozikabili haki za binaadamu na uhuru wa vyombo vya habari.