1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ripoti ya Ufaransa: Arafat hakufa kwa sumu

4 Desemba 2013

Uchunguzi uliofanywa na wanasayansi wa Ufaransa kuhusu kifo cha kiongozi wa zamani wa Palestina, Yasser Arafat, umeonyesha kuwa kiongozi huyo hakufa kutokana na sumu ya Polonium, bali alikufa kifo cha kawaida.

https://p.dw.com/p/1ASjn
Marehemu Yasser Arafat
Marehemu Yasser ArafatPicha: Getty Images

Kwa mujibu wa ripoti ya uchunguzi wa wanasayansi hao, vipimo vimeonyesha kuwa Arafat alikufa kutokana na uzee baada ya kupata maambukizi na sio kutokana na sumu ya polonium, ingawa wamesema kulikuwa na ishara za plotunium.

Matokeo hayo yanatofautiana na ripoti iliyotolewa awali na maabara moja ya Uswisi, iliyoeleza kuwa Arafat alikufa kutokana na kiwango kikubwa cha sumu ya polonium, baada ya kuigundua sumu hiyo kwenye nguo zake.

Ripoti hiyo ya Ufaransa imepingwa vikali na mke wa Arafat, Suha Arafat, ambaye amesema kifo cha mumewe kilikuwa ni mauaji ya kisiasa yaliyofanywa na mtu wake wa karibu. Akizungumza mjini Paris, Suha amesema ameshangazwa na taarifa zinazokinzana kutoka kwa waatalamu wa Ulaya.

Ripoti hiyo iliyokabidhiwa kwa Suha, haitachapishwa, lakini ofisi ya mwendesha mashtaka wa serikali imesema uchunguzi uliokamilika unaoonyesha kuwa Arafat hakuuawa kwa sumu ya polonium.

Arafat, aliyesaini makubaliano ya mjini Oslo ya mwaka 1993 na Israel, alifariki Novemba mwaka 2004 akiwa na umri wa miaka 75, katika hospitali moja nchini Ufaransa.

Kifo chake kilitokea wiki nne alipougua baada ya kula chakula na hivyo kusababisha kutapika na kuumwa tumbo. Taarifa za kitabibu zilionyesha kuwa alikufa kutokana na kutokwa damu katika ubongo, lakini hakukuwa na maelezo ya nini kilisababisha hali hiyo.

Palestina yapuuzia uchunguzi wa Ufaransa

Afisa mwandamizi wa Palestina, Wasel Abu Yousef, ameipuuza ripoti hiyo ya Ufaransa akisema kuwa iko kisiasa zaidi na iko kinyume na ushahidi unaothibitisha kuwa Arafat aliuawa kwa kupewa sumu.

Sumu ya Polonium iliyomuua jasusi wa Kirusi, Alexander Litwinenko.
Sumu ya Polonium iliyomuua jasusi wa Kirusi, Alexander Litwinenko.Picha: picture-alliance/dpa

Wapalestina wengi wanaamini kuwa Israel inahusika na kifo cha kiongozi wao, tuhuma ambazo Israel imezikanusha.

Mkuu wa kamati ya Palestina inayochunguza kifo cha Arafat, Tawfik Tirawi amesisitiza kuwa Israel inahusika na awali alisema atataja majina ya watu wanaoaminika kuhusika na kifo cha kiongozi huyo.

Hata hivyo, msemaji wa wizara ya mambo ya nje wa Israel, amesema kuwa ripoti ya matokeo ya Ufaransa si ya kushangaza na kuelezea matumaini yake kwamba sasa Arafat atapumzika kwa amani.

Mwaka uliopita, mjane wa Arafat aliitaka serikali ya Ufaransa ifanye uchunguzi wa kifo cha mumewe, baada ya kituo cha televisheni cha Al Jazeera kuripoti kwamba nguo za Arafat zilikutwa na sumu ya polonium.

Waendesha mashitaka wa Ufaransa walianzisha uchunguzi na hatimaye wataalamu wa kupekuwa ushahidi kutoka Uswisi, Urusi na Ufaransa, walichukua sampuli za mabaki ya mwili wa Arafat, baada ya kufukuliwa mwaka 2012.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/DPAE,APE,RTRE
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman