1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Safu za wahariri

12 Novemba 2008

Zimetuwama juu ya mkutano wa Bush na Obama,miaka 90 tangu vita vya dunia na jaa la taka za nuklia.

https://p.dw.com/p/FsS8
Obama na Bush(Ikulu)Picha: AP

Uchambuzi wa wahariri wa magazeti ya Ujerumani umegusia mada mbali mbali tangu za ndani hata nje: Mkutano wa Obama na Bush,ukumbusho wa jana wa vita vya kwanza vya dunia,ukumbusho wa mwaka wa 70 tangu Manazi katika kile kinachoitwa "Kristallnacht" "usiku wa vigae" pale wayahudi na mali zao walipohujumiwa humu nchini; msukosuko wa uchumi na jaa la taka za kinuklia la Gorleben.

Gazeti la Coburger Tageblatt na ziara ya Obama kwa George Bush Ikulu,mjini Washington laandika:

"Rais Bush anapaswa kutekeleza kile alichoahidi -yaani kumkabidhi hatamu mwenzake bila pingamizi.Kutimiza shabaha hiyo, anapaswa Bush kutomwekea mfuasi wake vizingiti vyovote vya kujikwaa na anapaswa pia kuheshimu kura ya raia.Hasa katika nyakati za misukosuko, changamoto za kukabiliana uso kwa uso hazifai.Ni kwa kuridhiana tu ndipo George Bush atafaulu kukumbukwa alao si mpinzani wa shujaa wa wapigakura."

Jana ilikua siku ya kutimu mwaka wa 90 tangu kumalizika vita vya kwanza vya dunia:Gazeti la Emder Zeitung lakumbusha:

"Ulikuwa msiba mkubwa wa karne ya 20-vita vilivyousumbua ulimwengu na kuhilikisha kizazi kizima cha vijana barani Ulaya. Vita hivyo jana vilikumbuka mwaka wake wa 90 tangu kumalizika.Ilikua siku ya kumalizika vita vilivyofungua mlango kwa vita vya pili vya dunia karne iliopita. Waingereza,wajerumani,wafaransa,wapoland na waakilishi wengi wa nchi nyengine walivikumbuka vita hivyo vya msiba mkubwa na vifo vingi-msiba uliosababishwa kati kati ya ulimwengu wa kiviwanda.Dola zikajikuta kwenye medani ya vita .sasa kutoka kuwa maadui ,sasa ni majirani wanaokutana kwa kuheshimiana.Yadhirika ,kwa mara nyengine walimwengu wamejifunza kutoka historia."

BILD-ZEITUNG linatuchukua katika ukumbusho mwengine usiofurahisha-kutimu mwaka wa 70 Novemba 9 tangu ule usiku wa kuteketeza mali za wayahudi -"kristalnacht":

Gazeti laandika:

"Novemba 9 ,Ujerumani na dunia zilitimiza wajibu wake-kuwahuzunia mayahudi kwa msiba uliowafika miaka 70 iliopita katika usiku wa vigae-kristalnacht.ilikua pia siku ya kuwakumbuka mayahudi milioni 6 waliohilikishwa na wasaidizi wa Adolf Hitler.

Hivi sasa wayahudi wanaishi miongoni mwetu wakilindwa uzuri.Hatahivyo, hatari ya kudhuriwa haikondoka kabisa..........Badala Novemba 9 kuwakumbuka mayahudi waliouwawa,inatupasa kuzuwia mauaji mapya.Na sio tu kwa wayahudi,bali hata kwa wakristu nchini Sudan.Kwani huko waislamu wenye itikadi kali wanawaadhibu watu milioni 2.Darasa la Novemba 9 ni hili:

"Zuwia mauaji ya halaiki kwa wahanga wowote wale kwa kadiri muda wa kufanya hivyo bado upo."

Gazeti la Westdeutsche zeitung linazungumzia malalamiko juu ya jaa la takataka za nuklia nchini Ujerumani.Linasema:

"Rasmi inasemwa linatafutwa jaa jengine la kuzitupa kabisa taka hizo za kinuklia.Hatua gani zimefikiwa katika kutafuta jaa hilo jengine iwapo kweli zimefanywa,haijulikani hadharani kwavile, mada hiyo ni nyeti.Yule lakini anaetaka kujadili mkasa huu kwa muda mrefu,anapaswa kusema wapi taka hizo zaweza bila kusababisha dhara kutupwa.Hatua za kusaka jaa hilo zapaswa kutiwa kasi na kuwekwa wazi kabisa hadharani."