1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sheria ya umilikaji silaha yaimarishwa Ujerumani

27 Mei 2009

Baraza la mawaziri limeidhinisha sheria kali zaidi:

https://p.dw.com/p/HyPc

Jumla ya watu 16 waliuliwa katika mkoa wa kusini mwa Ujerumani wa Baden-Wurtemberg hivi karibuni.Kijana mwenye umri wa miaka 17 aliwafyatuliwa wenzake risasi.Kisa hiki kilitokea mwezi Machi,mwaka huu.

Jana, zaidi ya miezi 2 baadae, Baraza la mawaziri la Ujerumani ,lilikutana mjini Berlin na kuafikiana vikwazo vikali zaidi vya kisheria ili kudhibiti umilikaji silaha.

Sheria hiyo ya kudhibiti umilikaji silaha imetiwa makali zaidi hata kabla ya uchaguzi mkuu ujao.kimsingi, sheria hiyo inaleta mabadiliko yafuatayo: Yule anaeweka silaha nyumbani mwake,atarajie kuanzia sasa ukaguzi wa ghafula wa polisi hata bila kuwapo sababu za shaka-shaka.Watakagua iwapo risasi,bunduki kama sheria inav yotaka zimefungiwa katika makabati ya chuma tena barabara.Makabati hayo yawe yamejengewa ukutani.

Bingwa wa maswali ya ndani na wa sheria wa vyama -ndugu vinavyotawala CDU/CSU Wolfgang Bosbach,anaamini kwamba, hapatazuka balaa lolote pale uchunguzi wa ghafula utapofanywa.

Anatoa sababu hii:

"Sababu ni wamiliki wa silaha wafuatao sheria,wanaotumia bunduki kutunga shabaha kispoti na wawindaji wanyama watakuwa n a hamu kubwa kudhihirisha kuwa majumbani mwao kila kitu kiko sawa kwa muujibu wa sheria."

Yule atakewazuwia polisi kuingia majumbani mwao kufanya ukaguizi kama huo,watarajie basi waweza wakapokonywa leseni ya kumiliki silaha zao.

Umri wa kuruhusiwa kumiliki bunduki za hali ya juu utapandishwa sasa kutoka miaka 14 na kuwa 18.Zaidi patakuwapo dafutari la kote nchini la kuwasajili na kuwatambua harakawale wenyekuruhisiwa kumiliki silaha.

Kwa kutiwa makali sheria ya umilikaji silaha nchini Ujerumani,kumetolewa kipindi maalumu cha msamaha ili kujirekebisha kwa wale wenye kumiliki silaha kinyume na sheria hii. Kwahivyo, yule anaemiliki silaha bila leseni anaruhusiwa hadi mwisho wa mwaka huu kuikabidhi polisi silaha yake bila kutazamia kuandamwa na kuadhibiwa.

Sheria zote katika mfumo huu mpya uliotiwa makali zaidi, utatoa usalama zaidi tu ikiwa kama asemavyo Bw.Rudolf Kłrper wa chama cha SPD anaehusika n a maswali ya ndani:

"Mtu akituuliza sasa -swali linalopendwa mno kuulizwa: baada ya kupitishwa sheria hii,visa kama hivyo vya ufyatuaji risasi vyaweza kuzuka tena? Kwa bahati mbaya yatupasa kujibu ndio yawezekana."

Azma ya awali ya kupiga marufuku michezo ya kupigana kama ile inayoitwa "painball, Gotcha au Laserdom",sheria hiyo haitapitishwa kwavile kuna shaka-shaka iwapo marufuku kama hayo yanakiuka katiba.Licha ya wasi wasi huo wa kukiukwa katiba,bingwa wa maswali ya ndani wa chama cha SPD Wiefelsputz anadai hakubadili maoni yake juu ya marufuku hayo.Anahisi mchezo wa kuigiza kuua kwa matumizi ya silaha au zana ,bunduki-bandia si mchezo mwema na unaokiuka utu wa mwanadamu na desturi zake.

Mwenyekiti wa chama cha walinzi wa mazingira-chama cha KIJANI bibi Claudia Roth anahisi mageuzi ya sheria hii iliopitishwa ya umilikaji silaha hayana maana yoyote:

"Bunduki hazistahiki kuwapo majumbani na kwamba silaha zinazoweza kuuwa zisiruhusiwe nchini mwetu kutumiwa kama hobi au mchezo wa kujitumbuiza."

Mtayarishaji: Ramadhan Ali

Mhariri: M.Abdul-Rahman