1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SIPRI: Matumizi ya fedha kijeshi yaongezeka

Isaac Gamba
2 Mei 2018

Matumizi ya fedha kijeshi yalipanda kwa kiwango cha  hadi dola tirilioni 1.7 ambacho ni cha juu zaidi  tangu kumalizika vita baridi huku Marekani, China na Saudi Arabia zikiongoza kwa matumizi hayo.

https://p.dw.com/p/2x0Od
Proteste gegen Reformen in Nicaragua
Picha: picture-alliance/AP Photo/A. Zuniga

Taasisi hiyo ya kimataifa inayohusika na utafiti wa masuala ya amani inakadiria  kiasi cha dola tirilioni 1.73 ziliwekezwa kwa ajili matumizi ya kijeshi pekee likiwa ni ongezeko la asilimia 1.1 kulinganisha na mwaka 2016  na hiyo ikimaanisha kuwa ni sawa na dola 230 kwa mtu mmoja.

Marekani imeendelea kuongoza kwa matumizi hayo ulimwenguni kote kwa kiwango cha dola bilioni 610 kiwango kinachoonekana kutobadilika mwaka hadi mwaka huku nchi hiyo ikihusishwa na zaidi ya robo ya matumizi ya fedha kijeshi duniani kote. 

Akihojiwa na DW mtafiti mwandamizi wa taasisi ya SIPRI  Pieter Wezeman amesema China ambayo inashika nafasi ya pili inakadiriwa kutumia kiasi cha dola bilioni 228 na matumizi yake yameongezeka kwa kiwango cha aslimia 5.6 ambacho ni cha juu katika kipindi cha kuanzia mwaka 2008.

Kwa upande mwingine Saudi Arabia imeshika nafasi ya tatu katika orodha hiyo ambayo awali ilikuwa ni nafasi ya Urusi na kwa mujibu wautafiti huo matumizi yake kijeshi yamefikia dola bilioni 69.4 kwa mwaka 2017.

Licha ya kushuka  bei ya mafuta migogoro ya kivita inayoendelea Mashariki ya Kati imechochea matumizi ya fedha kijeshi katika kanda hiyo.

 

Matumizi ya Urusi kijeshi yapungua

Ripoti hiyo ya SIPRI inaonesha mtumizi  ya Urusi kijeshi kupungua kulinganisha na mwaka 2016 ikiwa ni mara ya kwanza tangu mwaka 1998.  SIPRI  imehusisha kushuka kwa matumizi hayo na kuporomoka kwa bei ya mafuta.

 Hata hivyo kujiboresha kijeshi bado kunaendelea kusalia kuwa kipaumbele cha Urusi.

Pieter D. Wezeman, senior researcher at SIPRI
Pieter D. Wezeman, Mtafiti mwandamizi wa taasisi ya SIPRI.Picha: SIPRI

India imeipiku Ufaransa katika matumizi hayo na kushika nafasi ya tano ambapo kwa mujibu wa utafiti huo inaonekana kutumia karibu dola bilioni 64.

 Utafiti huo unaonesha kuwa mataifa manne miongoni mwa mataifa 15 yanayoongoza kwa matumizi hayo  yanatoka barani ulaya. Mataifa hayo ni Ufaransa, Uingereza, Ujerumani na Italia.

Mataifa mengine ambayo ni mongoni mwa kundi la nchi hizo 15 ni pamoja na Japan, Korea Kusini na Australia.

SIPRI inasema Algeria inaendelea kusalia kuwa nchi yenye matumizi makubwa kijeshi barani Afrika lakini matumizi yake yalishuka katika mwaka 2017 kutokana na kushuka kwa bei ya mafuta na gesi.

Matumizi hayo yemeongezeka  kwa zaidi ya asilimia 4 kwa nchi za Amerika ya Kusini  huku Argentina na Brazil zikichochea matumizi hayo.

Kwa mujibu wa taasisi hiyo ya SIPRI  matumizi hayo yamezingatia mishahara, gharama za uendeshaji , manunuzi ya silaha na vifaa vinginevyo pamoja na gharama za utafiti na maendeleo.

Mwandishi: Karsten Knipp-DW/DPAE

Mtafsiri: Isaac Gamba

Mhariri: Josephat Charo