1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sudan Kusini yapanga kuzifunga balozi zake kadhaa

Zainab Aziz Mhariri: Yusra Buwayhid
15 Juni 2019

Sudan Kusini inapanga kuzifunga balozi zake kadhaa kwa ajili ya kubana matumizi. Hatua hiyo inaweza kuathiri vibaya uhusiano kati ya nchi hiyo na Norway na Ufaransa.

https://p.dw.com/p/3KVFA
Südsudan Riek Machar  Salva Kiir
Picha: picture-alliance/AP/J. Patinkin

Hatua ya Sudan Kusini ya kutaka pia kuzifunga balozi zake za Norway na Ufaransa inaweza kuligharimu taifa hilo changa linalokabiliwa na matatizo katika mchakato wake wa amani na uchumi wake unaosuasua. Serikali ya mjini Juba imesema uamuzi wake huo ni kutokana na kuzorota kwa uchumi katika nchi hiyo ambayo bado inakabiliwa na ukosefu wa utulivu wa kisiasa.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje Mawien Makol aliiambia DW kwamba Sudan Kusini imechukua hatua ya kuzifunga balozi zake katika nchi za Ufaransa, Norway, Ghana, Kuwait na Italia,

Makol amesema masuala ya fedha ndio sababu za msingi zilizoifanya nchi yake kuchukua hatua hiyo ambayo wameamua kujaribu kufanya matumizi kwa busara kulingana na uwezo wan chi hiyo.  Msemaji huyo wa serikali ya Sudan Kusini amesema wanagharamia balozi zao kutokana rasilimali za nchi hiyo pamoja na fedha za misaada ya kuunga mkono mipango ya ujenzi baada ya nchi hiyo kutoka kwenye migogoro.

Norway inatoa mchango muhimu kwa Sudan Kusini na inatoa msaada wa kifedha kuchangia mchakato wa amani nchini humo. Norway inashirikiana na Marekani na Uingereza ni nchi zilizo mstari wa mbele katika kuwahimiza viongozi wa Sudan Kusini washirikiane ili kurejesha amani na utulivu nchini humo.

Rais wa Ufaransa Emmaanuel Macron
Rais wa Ufaransa Emmaanuel MacronPicha: Reuters/P. Wojazer

Ufaransa imekuwa nchi muhimu katika maamuzi ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa juu ya Sudan Kusini. Mwezi Mei 2019, Umoja wa Mataifa uliongeza vikwazo vya silaha dhidi ya nchi hiyo na pia dhidi ya maafisa kadhaa wa Sudan Kusini hasa baada ya kuzuka mapigano mapya.

Ufaransa ina kura ya turufu katika jumuiya hiyo ya kimataifa na inaweza kutumia nguvu yake katika Baraza la Usalama na kuishinikiza Sudan Kusini hatua ambayo siyo habari njema kwa serikali ya Juba.

Wachambuzi wa kisiasa wamesema kufungwa kwa balozi za Sudan Kusini kunaweza kuipunguzia nafasi nchi hiyo kwenye medani za kidiplomasia ambapo nchi hiyo imekuwa inafurahia hadi sasa na kuifanya itengwe kimataifa. Hatua hiyo inaweza pia kuharibu mahusiano na nchi zinazohisi kuwa zinatengwa na Sudan Kusini. Hatari hiyo ni kubwa kwa Norway na Ufaransa.

Chanzo:://p.dw.com/p/3KTsZ