1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Syria yakubali kuhamishwa kwa wanamgambo wa IS

Sekione Kitojo
27 Agosti 2017

Jeshi la Syria limeridhia, makubaliano kati ya kundi linalojiita Dola la Kiislamu na Hezbollah yanayoruhusu kuhamishwa wanamagmbo wa IS kutoka mpaka kati ya Syria na Lebanon kwenda mashariki mwa Syria.

https://p.dw.com/p/2iveN
Libanesische Armee startet Offensive gegen IS im Osten des Landes
Picha: Reuters/H. Abdallah

"Baada  ya  mafanikio  ya  majeshi  yetu  na  kundi  la  Hizbollah yaliyopatikana magharibi  mwa  Qalamoun , makubaliano yaliyofikiwa  kati  ya  Hezbollah  na  kundi  la  kigaidi  la  Daesh yameidhinishwa," televisheni  ya  Syria  imesema, ikinukuu chanzo kutoka  jeshini.

Bado  haifahamiki  iwapo makubaliano  hayo  yanajumuisha wanamgambo  wa  IS  ambao  wako  katika  upande  wa  Syria wa  mpaka pekee ama  katika  ardhi  pia  ya  Lebanon.

Libanon Grenzgebiet zu Israel Hisbollah Kämpfer
Mwanajeshi wa Hisbollah akilinda doria katika mpaka kati ya Lebanon na SyriaPicha: picture-alliance/AP Photo/H. Malla

Makubaliano  ya  kusitisha  mapigano  yalianza  kufanyakazi Jumapili asubuhi   katika  eneo  lililokuwa  linadhibitiwa  na  kundi  la  Dola  la Kiislamu  lililoko  katika  eneo  la  mpaka, ambako  wanamgambo wamekuwa  wakipigana  na  kundi  la  Hezbollah pamoja  na  majeshi ya  Syria  kwa  upande  mmoja  na  jeshi  la  Lebanon  kwa  upande mwingine.

Majeshi  ya  Lebanon yalitangaza  kusitisha  mapigano   katika mpaka  kati  ya  syria  na  nchi  hiyo  kuruhusu  majadiliano kufanyika  kuhusiana  na  wanajeshi  waliokamatwa  mateka  na kundi  la  IS.

Lengo  la  makubaliano  hayo  ya  kusitisha  mapigano  karibu  na mji  wa  Ras Baalbek ni "kuruhusu  awamu  ya  mwisho ya majadiliano  yanayohusiana  na  hatima  ya  wanajeshi  waliotekwa nyara," limesema  jeshi  la  Lebanon katika  taarifa.

Hatima ya wanajeshi waliokamatwa haijulikani

IS limekamata  wanajeshi 9 mwezi  Agosti  2014 baada  ya kushambulia  mji  wa  mpakani wa  Arsal. Hatima  ya  wanajeshi  hao waliokamatwa haijajulikani.Taarifa zinasema  huenda  wanajeshi  hao wameuwawa , baada  ya  kupatikana  miili  sita ya  wanajeshi hao, na  bado inatafutwa miili  ya  wanajeshi  wengine watatu.

Libanon Offensive gegen IS
Wanajeshi wa Lebanon nje kidogo ya mji wa Ras Baalbek nchini Lebanon wanaopambana na wanamgambo wa ISPicha: picture-alliance/AP Photo/Lebanese Army Website

Maafisa  wa  usalama  wa  Lebanon wanasema  miili  inayoaminika kuwa  ya  wanajeshi  waliotekwa  ilipatikana imezikwa  karibu  na mpaka  na  Syria.

Duru  za  usalama  zimelieleza  shirika  la  habari  la  Reuters kwamba  jeshi  la  Lebanon limeanza  majadiliano  ya  "upatanishi" leo Jumapili  kwa  ajili  ya  kuachiliwa  wanajeshi  hao.

Kaskazini  mashariki  mwa  Lebanon  kunashuhudiwa  mapigano makali  ya  vita  nchini  Syria, ambapo  kundi  la  IS  na  makundi mengine  ya  jihadi  yanaongeza  uwepo  wao  katika  eneo  hilo  la mpaka.

Majeshi  ya  Lebanon na  Syria  yalianzisha  mashambulio  kila  moja upande  wake  katika  eneo  hilo  linalodhibitiwa  na  IS wiki  mbili zilizopita. Majeshi  ya  Syria  yanasaidiwa  na   kundi  la  Washia  la Lebanon  la  Hezbollah katika  mapambano  hayo.

Majeshi  ya  Syria  na  Hezbollah, pia  yametangaza  kusitisha mapigano  katika  eneo  hilo  la  magharibi  mwa  Syria  la  Qalamoun ambalo  liko  mpakani, televisheni  ya  Hezbollah  ya  al-Manar iliripoti leo Jumapili.

Mwandishi:  Sekione  Kitojo / rtre

Mhariri:  Caro Robi