1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Taliban waua watu zaidi ya 17 mjini Kabul

Abdu Said Mtullya29 Juni 2011

Hali ya wasiwasi baada ya shambulio la Taliban mjini Kabul. Jee wazalendo wataweza kuulinda usalama wa Afghanistan?

https://p.dw.com/p/11lSB
Hoteli ya Inter Continental iliyoshambuliwa na Taliban jana usiku mjini KabulPicha: dapd

Watu wasiopungua 17 wameuawa kutokana na shambulio lililofanywa na Taliban kwenye hoteli mashuhuri ya mjini Kabul.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, wapiganaji hao wa Taliban walijipenyeza katika hoteli hiyo jana jioni.

Taarifa rasmi zimesema watu waliouawa walikuwa pamoja na Taliban sita waliofanya shambulio hilo. Wengine ni polisi na raia wawili wa kigeni. Watu10 pia walijeruhiwa katika shambulio hilo.

Washambuliaji wanane waliokuwa na roketi za kurushia magurunedi na silaha za aina nyingine walijipenyeza katika hoteli ya kifahari - Inter Continental mjini Kabul licha ya hoteli hiyo kuwa na ulinzi mkali.

Washambuliaji waliuliwa baadae na wanajeshi wa Nato waliotumia helikopta.

Shambulio la jana limefanyika wakati ambapo mkutano ulikuwa ufanyike kwenye hoteli hiyo kujadili mchakato wa kuyakabidhi mamlaka ya ulinzi kwa wazalendo wa Afghanistan.

Shambulio la jana pia limefanyika wiki moja tu baada ya Rais Obama kuutangaza mpango wa kuanza kuwaondoa wanajeshi wa Marekani kutoka Afghanistan hatua kwa hatua.

Kutokana na hoteli hiyo ya Inter Continental kuwa na ulinzi mkali na kutokana na taliban kufanikiwa kulifanya shambulio la jana usiku sasa pana mashaka iwapo vyombo vya usalama vya Afghanistan vitakuwa na uwezo wa kuulinda usalama wa nchi baada ya majeshi yote ya Marekani kuondolewa.

Mfanyakazi kwenye kitengo cha mapokezi katika hoteli hiyo amearifu kwamba washambuliaji kadhaa waliingia katika hoteli wakiwa na kanda za nyimbo za kivita za kitaliban na walimshambulia kila mtu waliemwona ndani ya hoteli. Watu mashuhuri walikuwapo kwenye hoteli wakati wa shambulio la jana usiku, ikiwa pamoja na wakuu wa mikoa waliokuwa wanajitayarisha kuuhudhuria mkutano uliokuwa ufanyike leo.

Mwandishi: Matthay Sabina/NDR / abdul-Mtullya

Mhariri: Abdul-Rahman