1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania yarejea nyumbani, Kenya bado yasubiri

Sekione Kitojo
2 Julai 2019

Timu mbili kutoka  eneo  la  Afrika  mashariki  Tanzania  na  Kenya zililazimika  kukubali  kipigo sawia  kila  mmoja  akibeba  mabao 3 bila majibu  kutoka  kwa  wapinzani  wao  katika  mchezo  wa  kundi C jana Jumatatu.

https://p.dw.com/p/3LR0E
Afrika-Cup 2019 | Kenia vs. Senegal
Picha: Reuters/S. Salem

Wakati Tanzania  ikichezea  kichapo cha  mabao 3-0 kutoka  kwa  Algeria, Kenya  nayo  ilikuwa  ikikaangwa  bila  mafuta na  Senegal  na  kukubali  kipigo  kama  hicho  cha  mabao 3-0. Wakati Tanzania  ambayo  haina  pointi  hata  moja  kutokana  na michezo  mitatu , ikifunga  vifago  na  kurejea  nyumbani , hatima  ya Kenya  bado  haijaamuliwa , kutokana  na  kupata  ushindi  wa mabao 3-2  dhidi  ya  Tanzania  wiki iliyopita. Kenya pamoja  na Afrika  kusini  sasa  zinasubiri michezo  ya  makundi  kumalizika  leo kuona  iwapo  ni  miongoni  mwa  timu nne  bora  zilizoshindwa ili kufuzu  kuingia  katika  duru  ya  mtoano  ya  timu  16 zilizosalia.

Afrika  kusini  iliyokuwa  katika  kundi D ilifungwa  bao 1-0 na Morocco  jana  jioni , wakati Nambia  ilikubali  kipigo  cha  mabao 4-1 dhidi  ya  Cote D'Ivoire.

Afrika-Cup 2019 | Tansania vs. Algerien
Tanzania wameondoka Misri bila pointi yoyotePicha: Getty Images/AFP/J. Soriano

Michezo  ya  leo  ni  ya  makundi  E na  F  ambapo  Benin  yenye pointi 2  itapambana  na  Cameroon  ambayo  imefikisha  pointi 4, ikiwa  inaoongoza  kundi hilo.  Guinea Bissau  yenye  pointi 1 tu kutokana  na  michezo miwili  inaumana  na  Ghana ambayo  katika mashindano  ya  mwaka  huu  imeonekana  kusua sua  na  hadi sasa  ina  pointi 2 tu sawa  na  Benin. Baada  ya  mapambano  hayo kundi E litaingia  uwanjani  kuoeshana  kazi, wakati Angola  ambayo hadi  sasa  imejinyakulia  pointi 2 , itaingia  dimbani  kuoneshana kazi  na  Mali  yenye pointi 4  na  inaongoza katika  kundi E. Mauritania  ambayo  ndio  mara  yake  ya  kwanza  kufuzu  katika mashindano  haya  ya  kombe  la  mataifa  ya  Afrika  katika  historia ya  nchi  hiyo inaumana  na  Tunisia.

Algeria haikuwateremsha  majogoo  wake  11 waliopambana  na Senegal  katika   mchezo  wa  kwanza na  kushinda  wiki  iliyopita lakini  waliweza  pia  kuishinda  Tanzania  kwa  mabao 3-0 mjini Cairo  jana na  kuchukua  usukani  wa  kundi C wakiwa  na  pointi 9. Hii  ina  maana  kwamba  Algeria  imeshinda  michezo  yake  yote mitatu  katika  kundi  hilo, wakati  Tanzania  ndio  timu pekee  dhaifu ambapo imepoteza  michezo  yake  yote  mitatu, ikirejea  mjini  Dar es Salaam  bila  pointi  na  mzigo  wa  mabao manane  wakati yenyewe ikizifumania  nyavu  mara  mbili  tu.

Senegal  inashika  nafasi  ya  pili  ikiwa  na  pointi  sita, Kenya ikichukua  nafasi  ya  tatu kwa  kuwa  na  pointi 3, na  Tanzania ikirejea  kwa  mara  ya  kwanza  katika  mashindano  hayo  baada ya  kukosekana  kwa  muda  wa  miaka  39 , ikiambulia  patupu na nafasi  ya  nne.

Kufuzu  kwa  Senegal  jana  kunaongeza  idadi  ya  timu  ambazo tayari  zimekwisha  fuzu  kuingia  katika  awamu  ya  mtoano kufikia timu 12, awamu  inayoanza  rasmi siku  ya  Ijumaa.

Wenyeji  Misri , Madagascar  ambayo imemshangaza  kila  mpenzi wa  kandanda  hadi  sasa , Algeria  na  Morocco zinasonga  mbele kama  washindi  wa  makundi  yao na  Uganda, Nigeria, Senegal  na Cote D'Ivoire zimeingia  katika  awamu  hiyo  kama  timu  zilizoshika nafsi  ya  pili.

Guinea  na  Jamhuri  ya  Kidemokrasi  ya  Congo zimefuzu  kuingia katika  duru ya  mtoano  kwa  njia ya  kuwa  timu  bora  zilizoshindwa.