1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tatizo la wakimbizi wa Irak nchini Jordan halizungumziwi

Josephat Charo18 Mei 2007

Wakimbizi wa Irak zaidi ya laki saba unusu wanaishi nchini Jordan. Licha ya takwimu hiyo tatizo la wakimbizi wa Irak nchini humo halizungumziwi rasmi huku ikiwa imetimia mwaka mmoja tangu waziri mkuu wa Irak, Nuri Al Maliki, alipoingia madarakani. Ripoti ya mwadhishi wetu Peter Philip, aliye mjini Amman nchini Jordan, inasomwa kwenu na Josephat Charo.

https://p.dw.com/p/CHks
Wakimbizi wa Irak nchini Syria
Wakimbizi wa Irak nchini SyriaPicha: AP

Ndani ya duka moja karibu na wizara ya mashauri ya kigeni ya Jordan mjini Amman bango la picha ya rais wa zamani wa Irak Saddam Hussein limetundikwa. Mwenye bango hilo bila shaka ni mkimbizi wa Irak ambaye hataki kuficha huruma zake za kisiasa. Katika kitongoji cha Rabi´a jina sawa na kitongoji cha mji mkuu wa Irak, Baghdad, wapishi Wairak wanawauzia vyakula wateja wao wa kiiraki kana kwamba wako kwao Irak.

Katika barabara za Amman wanawake wa Irak waaliovaa mabuimbaui na hijabu wanajaribu kuuza sigara, sio pakiti nzima bali moja moja, hali ya kila siku nchini Irak na Jordan ambayo tangu uvamizi wa Marekani imeendelea kubadilika. Jambo hili limegueka kuwa maudhi kwa wengi.

Inakadiriwa kuna Wairaki laki saba unusu nchini Jordan thuluthi moja kati yao wakiwa maskini hohehahe. Lakini hakuna anayelizungumzia rasmi tatizo la wakimbizi nchini humo. Pengine ni kwa sababu mtu atatakiwa kuchukua hatua za kuwasaidia na tayari juhudi zimeanza kuujulisha ulimwengu kuhusu tatizo hilo. Kamati ya shirika la msalaba mwekundu imetoa mwito jumuiya ya kimataifa itoe faranga za Uswisi milioni 15 kama msaada kwa wakimbizi wa Irak nchini Jordan, ingawa kufikia sasa ni fedha kidogo tu zilizokusanywa.

Shirika la msalaba mwekundu tawi la Ujerumani linaandaa kiwango kwa serikali ya mjini Berlin kuwasaidia wakimbizi wa Irak nchini Jordan. Alfred Hasenöhrl wa shirika la msalaba mwekundu mjini Amman Jordan anasema, ´Ni wazi kwamba kuna uchovu katika utoaji wa misaada ya kifedha kwa ajili ya Mashariki ya Kati katika kipindi cha miaka mingi ya mizozo katika aneo hilo. Na kwa upande mwingine hali ya wakimbi wa kiiraki ni tatizo tete la kibinadamu lisiloonekena.´

Tatizo la wakimbizi halionekani aidha kwa sababu raia wa Jordan au Wairaki wenyewe hawalizungumzii. Lakini athari zinaonekana na zitazidi kuwa mbaya hususan kwa waathiriwa.

´Tatizo linajitokeza ni kwamba hawawezi kujumulishwa katika mfumo wa afya na elimu. Na pia hawawezi kunufaika kutokana na misaada zaidi ya kijamii au masilahi yao kushughulikiwa.´

Hali ya Wairaki inazidi kuwa mbaya kwa kasi kubwa kwa sababu raslimali za kuwasaidia ni haba. Mabadiliko hayatarajiwi kupatikana nchini Irak na Jordan ambayo ni nchi ndogo na maskini, italazimika kuendelea kubeba mzigo. Pia matumaini ya wakimbizi kurejea aidha nchini mwao au kwenda katika nchi ya tatu ya uhamishoni ni hafifu.

´Matumaini haya bila shaka ni ya ushindi lakini ukweli wa mambo kwa wakati huu ni tofauti kabisa. Hakuna mwenye matumaini ya hali nchini Irak kuboreka katika kipindi kifupi au kirefu kijacho ili wakimbizi waweze kurejea makwao. Na pia kufikia sasa ni mataifa machache sana yaliyolegeza sheria za utoaji wa visa kwa Wairak hivi kwamba uwezekano wa idadi kubwa ya wakimbizi kuhamia katika nchi ya tatu haupo.´

Mbali na wakimbizi laki saba unusu walio Jordan, Syria ina wakimbizi takriban milioni moja kutoka Irak. Alfred Hasenöhrl anasema suluhisho sio kuwatafutia nchi ya tatu ya uhamisho au kuwajengea makaazi mapya.

´Nadhani cha muhimu kutambua tatizo la wakimbizi lipo na hatua za makusudi zichukuliwe kutoa ushauri na kuwashughulikia masilahi yao katika nchi wanamoishi.´

Tatizo ndani ya Irak sharti litanzuliwe kwanza ili wakimbizi waweze kurejea makwao.