1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TCRA yawaonya raia kutosambaza taarifa za COVID-19

 George Njogopa15 Desemba 2020

Mamlaka ya Mawasiliano nchini Tanzania, TCRA, imeanza kusambaza ujumbe kuwaonya wananchi dhidi ya usambazaji wa taarifa zinazohusiana na janga la corona.

https://p.dw.com/p/3mjh8
Francis Mihayo
Picha: DW/D. Bulendu

Hatua hiyo inafuatia wasiwasi unaanza kujitokeza kwa baadhi ya wananchi kudai kuwa wimbi jipya la maambukizi ya ugonjwa huo limeanza kujitokeza nchini humo. 

Katika ujumbe wake kwa umma, TCRA inawataka wananchi kutosambaza taarifa zozote kuhusiana na janga hilo ikisema yeyote atayebainika atachukuliwa hatua kali.

Ujumbe huo ambao unasambazwa kupitia mitandao ya kijamii unatoa maelekezo kwa wananchi hatua wanazopaswa kuchukua pindi wanapokutana na taarifa kuhusiana na janga hilo la corona.

Sehemu ya ujumbe huo inasema: "Ukipokea, au ukiona ujumbe unaochochea, kuzusha au kupotosha taarifa za corona katika kundi lako au lolote lingine mtandaoni piga picha ujumbe huo na namba ya aliyetuma utume TCRA." Mwisho wa kunukuu.

Mamlaka hiyo imewahimiza wananchi kujiepusha na kile inachosema ni udanganyifu na kuwasisitizia kuwa watumie uwanja wa mawasilino kwa ajili ya kujiletea maendeleo na wala siyo vinginevyo.

Tangazo la TCRA linakuja katika wakati ambapo kuna minong'ono inayozidi kuendelea kuhusiana na kurejea tena kwa maambukizo ya virusi vya corona hapa nchini.

Tansania Wahlkampagne John Magufuli Rede in Dar es Salaam
Rais wa Tanzania John MagufuliPicha: Reuters/S. Said

Baadhi ya taarifa zinazoendelea kusambaa mitandaoni zinasema huenda janga hilo likawa limerejea upya nchini lakini hadi sasa hakuna mamlaka yoyote za serikali zilithibitisha juu ya hilo.

Hata hivyo, wafuatiliaji wa mambo wamekosoa hatua iliyochukuliwa na TCRA wakisema mamlaka hiyo inajaribu kubana uhuru wa wananchi kujadili kile wanachokijua. Sammy Ruhuza, mchambuzi anayeishi jijini Dar es Salaam ameiambia DW kwamba TCRA haipaswi kuwachagulia wananchi kipi cha kujadili:

Tanzania inasalia kuwa nchi pekee katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara ambayo imetangaza waziwazi kulishinda janga la corona kupitia maombi pamoja na kutumia dawa za asili. Ingawa baadhi ya watu ndani na nje ya nchi wanainyooshea kidole serikali kwa kuficha ukweli, hata hivyo serikali haijalegeza msimamo wake kuhusu kutokuwepo kwa maambukizo ya corona.

Mara ya mwisho wakati akizungumzia janga hilo, Rais John Magufuli alisema anaamini Mungu amejibu maombi ya Watanzania na amewanusuru na janga hilo linaloendelea kusumbua duniani kote.

Tanzania iliacha kutoa takwimu za wagonjwa wa Covid 19 tangu Aprili 29 mwaka huu iliposema hadi wakati huo watu waliokuwa wameambukizwa walikuwa 480 wakati waliopoteza maisha walikuwa 16.