1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump anaashiria ushindi wa mapambano dhidi ya IS

Oumilkheir Hamidou
7 Februari 2019

Rais Donald Trump anaashiria wafuasi wa itikadi kali wa Dola la Kiislam-IS watapokonywa ardhi yote wanayoidhibiti nchini Iraq na Syria. Matamshi hayo ameyatoa katika mkutano ulioitishwa katika wizara ya mambo ya nje

https://p.dw.com/p/3Ctoi
US-geführte Koalition gegen ISIS | F-22 Raptors
Picha: picture-alliance/Photoshot/U.S. Air Force/Senior Airman J. A. Hoskins

Rais Donald Trump amewaambia wawakilishi wa muungano wa mataifa 79 yanayoongozwa na Marekani katika mapambano dhidi ya  wafuasi wa itikadi kali wa Dola la Kiislam au Daesh kwamba wanamgambo hao wanadhibiti sehemu ndogo tu ya ardhi wanayodai kuwa ni ya utawala wao au Khalifa:"Wanajeshi wa Marekani, washirika wetu na vikosi vya kidemokrasi nchini Syria wameikomboa takriban ardhi yote iliyokuwa hapo awali ikidhibitiwa na IS nchini Syria na Iraq. Kimsingi habari hizo huenda zikatangazwa wakati wowote kutoka sasa, pengine wiki inayokuja, kwamba tunadhibiti asili mia kwa mia ya ardhi  au Khalifat. Lakini nataka kusubiri hadi tamko rasmi . Sitaki kulisema kabla."

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani Mike Pompeo
Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani Mike PompeoPicha: picture-alliance/dpa/AP Photo/A. Brandon

Marekani inashikilia mpango wa kuwarejesha nyumbani wanajeshi

Maafisa wa Marekani walisema IS wamepoteza asili mia 99.5 ya ardhi yao na kwamba wanadhibiti chini ya kilomita za mraba 5 nchini Syria, katika vijiji vya bonde la mto Euphrates.

Hata hivyo kuna hofu, uamuzi wa kuondolewa wanajeshi wa Marekani usije ukavuruga matumaini hayo. Rais Trump amewaambia washirika katika mapambano dhidi ya IS waliokutana katika wizara ya mambo ya nchi za nje kwamba ingawa "idadi ndogo ya waliosalia kutoka kundi hilo bado ni hatari" hata hivyo ameamua kuwarejesha nyumbani wanajeshi wa Marekani. Amewatolea wito washirika wasimame kidete na kuchangia ipasavyo katika mapambano dhidi ya ugaidi.

Kambi zinazowahifadhi wasyria wanaokimbia mapigano ya IS
Kambi zinazowahifadhi wasyria wanaokimbia mapigano ya ISPicha: picture-alliance/Zuma/J. Mohammad

Wanamgambo wasiopungua 5000 wa IS wamejificha Syria

Hata baada ya rais Trump na waziri wake wa mambo ya nchi za nje Mike Pompeo kutetea umuhimu wa kuwarejesha nyumbani wanajeshi wa Marekani, uamuzi uliowashitua washirika wao na kupelekea waziri wa ulinzi Jim Mattis kujiuzulu baadhi ya wakuu wa kijeshi bado wana wasi wasi.

Wanaharakati wanaofuatilia kwa makini mzozo nchini Syria wanazungumzia  dalili za kuongezeka uasi. Rami Abdulrrahman anaeongoza shirika lenye makao yake nchini Uingereza la kusimamia masuala ya haki za binaadam nchini Syria anasema IS bado wana wapiganaji kati ya 4000 hadi 5000 na wengi wamejificha misituni na milimani.

Umoja wa Mataifa pia umechapisha ripoti inayowataja IS kuwa "kitisho kikubwa cha magaidi ulimwenguni."

 

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AP

Mhariri: Iddi Ssessanga