1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump arejea kwenye kampeni baada ya kupona COVID-19

13 Oktoba 2020

Rais Donald Trump wa Marekani amerejea tena kwenye kampeni za uchaguzi mkuu kwa kufanya mkutano wa kwanza jimboni Florida siku kadhaa tangu alipogundulika na maambukizi ya virusi vya corona.

https://p.dw.com/p/3jpSR
USA I Donald Trump I Wahlkampf Florida
Rais Donald Trump wa Marekani akiwa mjini Sanford, FloridaPicha: Joe Raedle/Getty Images

Rais Trump aliwasili kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika eneo la wazi huko Sanford; Florida bila ya kuvaa barakoa.

Mkutano wa kampeni mjini Florida,  jimbo ambalo ni muhimu kwa Trump kushinda, unafungua njia ya mikutano zaidi iliyopangwa kufanyika wiki hii kwenye majimbo ya Pennsylvania, Iowa na North Carolina. 

Akiwahutubia maelfu ya wafuasi wake waliosimama bega kwa bega wengi wakiwa bila barakoa, Trump amesema afya yake imeimarika na yuko huru kukutana tena na wapiga kura bila ya kuwa na wasiwasi wowote.

 "Nimetiwa nguvu kwa maombi yenu na nimefarijika kwa uungaji wenu mkono. Tunaungwa mkono vya kutosha. Na tuko hapa lakini tunaenda kukamilisha, tutalifanya taifa hili kuwa kubwa kuliko ilivyokuwa hapo kabla." alisema rais Trump.

Siku 10 za kupambana na virusi vya corona .

USA Präsident Trump im Walter Reed Hospital
Rais Trump alikuwa hospitali kutibiwa viruis vya corona Picha: Joyce N. Boghosia/The White House/Reuters

Trump anayewania muhula wa pili katika uchaguzi wa Novermba 3, alilazimika kukatiza kampeni yake kwa karibu siku 10 kufuatia kuambukizwa virusi vya corona mnamo Oktoba 2.

Kurejea kwa mikutano yake ya kampeni kunafanyika ikiwa ni wiki tatu kabla ya uchaguzi mkuu  na Trump anataka kubadili mwelekeo wa kinyang´anyiro hicho baada ya kura za maoni ya umma kuonesha anapoteza uungwaji mkono kwenye baadhi ya majimbo kwa mpinzani wake Joe Biden wa Democrats

Maswali kuhusu hali ya afya yake bado yanaendelea lakini daktari wa kiongozi huyo amesema kipimo alichofanyiwa rais Trump hivi karibuni kimeonesha hana tena maambukizi ya virusi vya coronana anaruhusiwa kusafiri.

Msimamo wake kuhusu COVID-19 haubadiliki 

USA Washington Weißes Haus | Donald Trump, Präsident
Picha: Alex Brandon/AP Photo/picture-alliance

Hata hivyo mkutano wake mjini Sanford umeonesha wazi kuwa Trump hajabadili mtindo wake wa kampeni hata baada ya yeye mwenyewe kuambukizwa virusi vya corona ambavyo tayari vimewauwawa watu 214,000 na kuambukiza  wengine milioni 7.8 nchini Marekani.

Trump aliwaambia wafuasi wake mjini Sanford kuwa vizuizi vilivyowekwa kukabiliana na kusambaa virusi vya corona vimefanya uharibifu mkubwa kwenye uchumi na vilikuwa vikali kupita kawaida.

Wakosoaji wanamlamu Trump kwa kushindwa kuwahimiza wafuasi wake na wafanyakazi wa ikulu ya White House juu ya umuhimu wa kuvaa barakoa na kuhehsimu kanuni za kujitenga.

Kwa miezi kadhaa Trump alijitahidi kuhamisha mjadala wa umma kuhusiana na jinsi alivyoshughulikia suala la viruis vya corona.

Lakini kisa cha yeye kuuambukizwa virusi kimefanya iwe muhimu kutizama kile serikali yake ilifanya kupambana na janga hilo na mpinzani wake Joe Biden anatumia vizuri nafasi hiyo kwa kumkaba koo Trump na kumshambulia kwa kutshughulikia kadhia ya corona kwa umakini.