1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump ataka ushirikiano mpya kiuchumi na nchi za APEC

Isaac Gamba
10 Novemba 2017

((Rais wa Marekani Donald Trump amewaeleza viongozi wanaoshiriki katika mkutano wa kilele wa ushirikiano wa kiuchumi wa nchi za Asia na Pasifiki, APEC kuwa Marekani imepata changamoto katika mikataba iliyopita.

https://p.dw.com/p/2nOl4
USA Donald Trump Rede beim APEC Gipfel in Danang
Picha: Reuters/A. Wallace

Akizungumza katika mkutano huo Trump aliulaumu utawala wa Marekani uliopita  kwa kuruhusu hali hiyo kukuwa na kuendelea ikiwa ni pamoja na baadhi ya mataifa barani Asia yakiongozwa na China kuwa na nguvu zaidi katika soko huru la biashara  na kuua soko la ajira nchini Marekani.

Trump ametolea mfano taifa la China na mengineyo kwa kuingia mikataba ya kibiashara inayolenga kuyanufaisha zaidi mataifa hayo na kuyawezesha kuuza zaidi bidhaa zake nchini Marekani kuliko yanavyoingiza bidhaa katika mataifa yao.

Trump ameongeza kuwa kwa sasa anafikiria kuanzisha ushirikiano mpya wa kibiashara na mataifa ya nchi za Pasifiki kwa kuingia mikataba ya kibiashara na nchi ambazo zitakuwa tayari kuheshimu makubaliano ya mikataba hiyo kwa masilahi ya pande zote.

Trump ameuleza mkutano huo wa kilele kiuchumi wa nchi za Asia na Pasifiki kuwa sasa atahakikisha Marekani na nchi wanachama wa APEC wanakuwa washirika kibiashara  kwa muda mrefu huku pia akipongeza mafanikio ya kiuchumi yaliyokwishapatikana hadi sasa.

Aidha Trump ametoa mwito kwa makampuni binafisi ya kibiashara kuwa na nafasi kubwa katika kujihusisha na mikataba hiyo ya kibiashara na kukosoa hatua ya serikali kuingilia zaidi masuala ya kibiashara. 

 

Asema Marekani haikutendewa haki na WTO

Vietnam - Gipfels des Asiatisch-Pazifischen Wirtschaftsforums Apec in Hanoi
Baadhi ya viongozi wanaoshiriki mkutano wa APECPicha: Getty Images/AFP/Kham

Amesema pia kuwa Marekani haikutendewa vema na shirika la kibiashara ulimwenguni  (WTO) na kusema mara nyingi baadhi ya mataifa ambayo yamekuwa hayaheshimu misingi ya shirika hilo yamekuwa yakinufaika zaidi kibiashara kwa kutumia mgogongo wa Marekani.

Rais  Donald Trump ambaye anaongozana na mkewe Mellania katika ziara hiyo barani Asia amesisitiza kuwa siku zote ataendelea kuipa kipaumbele kwanza Marekani kuliko kitu kingine chochote na kuyataka pia mataifa mengine kuiga mfano huo kwa kutanguliza masilahi ya nchi zao kwanza.

Waziri wa masualaya uchumi wa Japan Toshimitsu Motegi amesema baadhi ya wajumbe katika mkutano huo waliakubaliana kimsingi juu ya kuuufanyia maboresho mkataba wa ushirikiano huo ingawa alisema hana hakika kama hilo litakubaliwa na pande zote.

Wakati wa ziara ya sikummbili nchini China , Trump na rais wa China Xi Jinping walitangaza kuingia mikataba ya ushirikiano kibiashara kati ya nchi hizo mbili yenye thamani ya  dola bilioni 250.

Rais Donald Trump yuko katika ziara ya siku 11 barani Asia ikiwa ni ziara yake ya  kwanza barani humo  tangu ashike

madaraka ya urais ambayo imemuwezesha kuzuru Japan, Korea Kusini na China.

Mwandishi : Isaac Gamba/dw/ape

Mhariri: Josephat Charo