1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump avishambulia vyombo vya habari Arizona

Yusra Buwayhid
23 Agosti 2017

Rais wa Marekani, Donald Trump, ametetea matamshi yake ya baada ya ghasia za Charlottesville na kuvilaani vyombo vya habari kwa kutokuwa na uaminifu, katika mkutano huko Arizona. Maelfu ya raia pia waliandama kumpinga.

https://p.dw.com/p/2igOy
USA Präsident Donald Trump in Phoenix
Picha: Reuters/A. Brandon

Trump alikabiliwa na kauli za hasira baada ya kusema kwamba anazilaumu 'pande nyingi' kwa ghasia zilizotokea Charllotesville Virginia, zilizosababisha kifo cha mwandamanaji aliyekuwa akipinga ufashisti.

Akirudia tena matamshi yake aliyoyatoa kufuatia ghasia hizo za Charlottesville, Trump akiwa mjini Phoenix, Arizona, alivilaumu vyombo vya habari kwa kumtafsiri vibaya.

" Watu pekee wanaotoa jukwaa kwa vikundi hivi vya chuki ni vyombo vya habari, pamoja na habari za uongo," amesema Donald Trump.

Hotuba hiyo ilikuja mwishoni mwa ziara ya Trump katika jimbo la Arizona, ambayo ikulu ya Marekani - White House- ilitarajia kuwa itawashawishi zaidi wafuasu wa Trump na kuongeza kasi juu ya mpango wenye utata wa kujenga ukuta katika mpaka kati ya Marekani na Mexico.

Pia kulikuwa na wafuasi wa Trump, waliokuwa wakipiga mayowe ya kutaka kujengwa kwa ukuta huo. Wengi walivalia kofia nyekundu yenye kauli mbiu ya kampeni ya Trump ya wakati wa uchaguzi uliopita, inayosema "jenga tena Marekani iliyo bora”

Trump aligusia masuala mengi

Rais wa Marekani pia aligusia juu ya uwezekano wa kumsamehe Joe Arpaio, mkuu wa polisi wa zamani aliyehukumiwa mwezi uliopita katika kesi inayohusu makosa ya ubaguzi wa rangi.

Arpaio, aliyekuwa mkuu wa polisi wa kaunti ya Maricopa huko Phoenix kabla ya kushindwa katika uchaguzi mpya mwaka 2016. Ni mpinzani mkubwa wa uhamiaji kinyume cha sheria. Arpaio mwenye umri wa miaka 85 pia alijulikana kwa kuchunguza hati ya kuzaliwa ya rais wa zamani wa Marekani, Barack Obama, na kudai bila ya ushahidi wa msingi kwamba hati hiyo ilikuwa ya uwongo.

USA Proteste gegen Donald Trump in Phoenix
Maandamano yaliyofanyika Phoenix dhidi ya Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: picture-alliance/AP Photo/M. York

Trump alianza siku yake katika mji Yuma kwa kutembelea kituo cha operesheni za doria za mpakani alikozungumza na walinzi wa mpakani. Baada ya hapo Trump alielekea mji wa Phoenix kwa mkutano uliofanana na wa kampeni ambapo alitambulishwa kwa umati wa watu Makamu wa Rais Mike Pence.

Trump pia aligusia masuala mengine kadhaa ikiwa ni pamoja na makubaliano ya biashara ya mataifa ya Amerika Kaskazini (NAFTA), mvutano kati ya Marekani na Korea Kaskazini na mambo mengine kadhaa katika hotuba hiyo iliyochukuwa takriban saa moja na dakika 15.

Wakati hayo yakijiri, maelfu ya watu waliandama nje ya eneo alipokuwa akihutubia Trump kumpinga rais wao. Polisi waliwatawanya kwa kutumia kemikali ya kuwasha baada ya kurushiwa mawe na chupa na waandamanaji hao.

Idadi kamili ya watu waliojitokeza katika maandamano hayo haikuwekwa wazi na maafisa wa polisi lakini vyombo vya habari vya Arizona vimesema vimekadiria watu hao walikuwa kwa maelfu.

Watu wanne walitiwa mbaroni na polisi wakati wa maandamano hayo, watatu kati yao kwa madai ya kufanya mashambulizi, amesema mkuu wa polisi ya Phoenix, Jeri Williams, wakati wa mkutano na waandishi habari.

 

 

Mwandishi: Yusra Buwayhid/rtre,afpe.

Mhariri: Iddi Ssessanga