1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump kuiondoa Marekani kutoka mkataba wa nyuklia na Urusi

Sekione Kitojo
21 Oktoba 2018

Rais donald Trump amesema siku ya Jumamosi(20.10.2018) kwamba  Marekani itajitoa  kutoka  mkataba  wa  enzi za vita baridi ambao unafuta aina ya silaha za nyuklia kutokana na ukiukaji unaofanywa na Urusi.

https://p.dw.com/p/36u3l
Symbolbild USA-China-Handelskrieg
Picha: Colourbox

Hatua  hiyo  imeelezwa  na  afisa mmoja  wa  Urusi kuwa  ni  jaribio  hatari  la kuibana nchi  hiyo.

Mkataba unaojulikana kama Intermediate-Range Nuclear Forces Treaty, uliojadiliwa na  kufikia  makubaliano wakati wa  utawala  wa rais Ronald Reagan  na  kiongozi  wa  Urusi wakati  wa enzi za Umoja  wa  kisovieti Mikhail Gorbachev  mwaka  1987, unataka kuondolewa  kabisa  kwa  makombora  ya  kinyuklia  ya  masafa mafupi na  kati  pamoja  na  makombora  ya bara  hadi  para kwa nchi  zote.

USA Elko  Trump Statement
Rais Donald Trump wa MarekaniPicha: Reuters/J. Ernst

"Urusi  kwa  bahati  mbaya, haijatimiza  makubaliano  hayo  kwa  hiyo tutasitisha  makubaliano  hayo  na  tutajitoa," Trump  aliwaambia waandishi  habari  baada  ya  mkutano  wa  hadhara  mjini  Nevada.

Washington  inaamini  serikali  ya  mjini Moscow  inatengeneza  na imeweka  mfumo  wa kurusha  makombora  wa  ardhini  ambao  ni ukiukaji  wa  mkataba  huo  wa  INF ambao  ungeweza  kuruhusu Urusi  kufanya  mashambulio  ya  nuklia  katika  mataifa  ya  Ulaya muda  mfupi sana wakitaka.

Urusi yakana

Urusi imekuwa  ikikana ukiukaji wowote  kama  huo.

Symbolbild Geisterzug Russland
Kombora la Urusi likisafirishwa wakati wa mazoweziPicha: Getty Images/AFP/N. Kolesnikova

Trump  amesema  Marekani  itatengeneza silaha  hadi  pale  Urusi na  China  zitakapokubali kusitisha  utengenezaji.

China haimo  katika  mkataba  huo  na  imewekeza kwa kiasi kikubwa katika  makobora ya masafa marefu  kama sehemu  ya mkakati wa  kuzuwia kuingiliwa  katika  maeneo  yake, wakati mkataba  wa  INF umepiga  marufuku Marekani  kuwa  na makombora ya  masafa  marefu  yanayorushwa  kutokea  ardhini ama  makombora  yenye uwezo  wa  kurushwa  kwa  umbali  wa kilometa 500  na  5,500.

Mshauri  wa  usalama  wa  taifa  wa  Trump , John Bolton , atakwenda  Moscow  wiki  ijayo.

Naibu  waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Urusi , Sergei Ryabkov, katika  matamshi  yaliyoripotiwa  na  shirika  la  habari  la  Urusi TASS, amesema  hatua  ya  Marekani  kuchukua  uamuzi  wa kujitoa bila makubaliano  na  upande  wa  pili "itakuwa  hatua  ya  hatari sana."

Russland Wladimir Putin beim Valdai Forum in Sotschi
Rais wa Urusi Vladimir PutinPicha: picture-alliance/dpa/Sputnik/S. Marmontov

Ryabkov pia  amenukuliwa  akisema  kwamba  ni  Marekani  na Urusi  ambazo zinashindwa  kutekeleza   mkataba  huo.

Amesema  utawala  wa  Trump  unatumia  mkataba  huo  katika jaribio la  kuikandamiza serikali  ya  Urusi, na  kuuweka  usalama  wa dunia  katika  hatari.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / rtre

Mhariri: Zainab Aziz