1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump na Erdogan waahidi ushirikiano zaidi

Sylvia Mwehozi
17 Mei 2017

Rais Donald Trump wa Marekani na mwenzake Recep Tayyip Erdogan walisimama bega kwa bega  katika Ikulu ya Marekani White House siku ya Jumanne(16.05.2017) na wakaahidi kuimarisha mahusiano yao.

https://p.dw.com/p/2d5fS
Erdogan und Trump USA
Picha: Reuters/K.Lamarque

Hatua hiyo inakuja licha ya kiongozi huyo wa Uturuki kuonya hatua ya Washington kuliunga mkono kijeshi kundi la wanamgambo wa Kikurdi. 

Akiwa ndio kwanza ametoka katika kikaango cha kura ya maoni ya kutanua mamlaka yake, Erdogan ameitembela Ikulu ya  Marekani akiwa na malalamiko kadhaa juu ya Marekani kuwaunga mkono wapiganaji wa Kikurdi na kile Ankara inachosema kwamba Washington ndio ilikuwa mpangaji mkuu wa mapinduzi yaloshindwa.

Lakini viongozi wote wawili walijitahidi kuonesha nyuso za kijasiri juu ya tofauti zao na kufanya upya muungano muhimu baina ya mwanachama wa NATO aliye na nguvu na mwanachama wake mkubwa wa kiislamu, washirika katika mapambano ya kuliangamiza kundi la Dola la Kiislamu nchini Syria na Iraq.

"Tumejizatiti kupambana na namna zote za ugaidi bila ya ubaguzi ama kitu kingine chochote ambacho kinaonekana kuwa kitisho katika wakati wa sasa na huko mbeleni. Hakuna namna ya kuruhusu uwepo wa taasisi yoyote ya kigaidi katika mustakabali wa mbele wa ukanda wetu," amesema Rais Tayyip Erdogan.

Washington Pro-Erdogan Demonstranten im  Lafayette Park
Wafuasi wa Erdogan wakibishana na wale wanaompinga rais huyo mjini Washington.Picha: Reuters/J. Ernst

Trump alikuwa miongoni mwa viongozi wa kwanza kumpongeza Erdogan baada ya kushinda kura ya Aprili 16 ya kuimarisha mamlaka yake na mwenzake huyo wa Uturuki alilipa pongezi  hizo hapo jana siku ya Jumanne kwa kumsifu mwenyeji wake kwa "hadithi ya ushindi" wakati wa mbio za urais.

Trump aliipongeza Uturuki katika mchango wa kihistoria ilioutoa kwa muungano wa magharibi wakati wa vita ya baridi na kusema kwamba,"leo tunakabiliana na adui mpya katika mapambano ya ugaidi na tena tunataka kukabiliana na kikwazo hiki kwa pamoja. Watu wa Uturuki wamepatwa na mashambulizi mabaya ya ugaidi katika miaka ya nyumai na hata hivi karibuni," amesema Rais Trump.

Washington na Ankara wanapingana vikali juu ya uungaji mkono wa Marekani kwa kundi la wapiganaji la YPG nchini Syria ambalo linafanya kazi kama jeshi kuu la ardhini katika mipango ya Pentagon ya kuliangamiza kundi la IS lakini Uturuki inaliona kundi hilo kuwa la kigaidi na lenye mahusiano na kundi lililopigwa marufuku la chama cha wafanyakazi wa kikurdi PKK.

Erdogan angali bado na hasira kwamba Marekani inamhifadhi Fethullah Gulen, mshirika wa zamani ambaye anaishi uhamishoni Pennsylvania na ambaye anatuhumiwa kwa hivi sasa kwamba ndiye aliyepanga jaribio la mapinduzi nchini mwaka.

Baada ya Erdogan kuondoka Ikulu ya white House, mvutano kuhusu suala la wakurdi lilisambaa nje ya mitaa ya ya Washington wakati kiongozi huyo alipokwenda kumtembelea balozi wa Uturuki kwa Marekani. Watu wawili wamekamatwa baada ya wafuasi wa Erdogan na walinzi kukabiliana na waandamanaji wa kikurdi na wamarekani ambao wanamtuhumu kiongozi huyo kwa ukiukwaji wa haki.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi

Mhariri: Saumu Mwasimba