1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tuhuma za udanganyifu zautia dosari uchaguzi wa Msumbiji

Saumu Mwasimba
16 Oktoba 2019

Chama tawala cha Frelimo kinatuhumiwa kufanya udanganyifu kwenye uchaguzi na kutowa vitisho dhidi ya wapiga kura wa chama cha upinzani.Kura zimeanza kuhesabiwa na matokeo ya mwanzo yatarajiwa Alhamisi

https://p.dw.com/p/3RN4h
Wahlen in Mosambik Maputo
Picha: Reuters/G. Neuenburg

Uchaguzi nchini Msumbiji umefanyika katika mazingira ya utulivu kiasi, lakini kituo cha umma cha masuala ya uadilifu CIP kimetowa ripoti inayosema, uchaguzi huo umekumbwa na taarifa za masanduku kujazwa kura kabla hata ya zoezi la upigaji kura pamoja na kuzuiwa kwa waangalizi kufanya kazi zao.

Kituo cha kusimamia uadilifu CIP kinasema wajumbe wake wameripoti visa vya kutokea jaribio la masanduku ya kura kujazwa kura  na kwamba kuna watu kadhaa waliokamatwa wakiwa na karatasi za ziada za kupigia kura ambazo zilikuwa zimeshajazwa jina la chama cha Frelimo na mgombea wake wa urais.

Mosambik, Maputo: Menschen warten vor einem Wahllokal
Picha: Getty Images/AFP/G. Guercia

Chama tawala cha Frelimo kimetuhumiwa kufanya udanganyifu katika orodha ya wapiga kura waliojiandikisha katika ngome zake. Kituo cha CIP pia kinadai yalikuwepo pia majaribio ya kuwazuia waangalizi huru wa uchaguzi kufanya kazi zao kwa kuwanyima vibali vya kuingia kwenye maeneo ya upigaji kura katika mikoa kadhaa. Kuna mikoa 11 ambayo imetajwa kuwa ni karata muhimu iliyobadilisha mambo katika uchaguzi huu ambapo imeshuhudiwa chama cha Upinzani kitakuwa na fursa ya kuchagua magavana katika mikoa ambako wanashinda kura nyingi zaidi.

Ikumbukwe kwamba hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa kipindi cha miaka 40 ya utawala wa chama cha Frelimo,upinzani unapata nafasi hii ya kuchagua magavana kwenye mikoa hiyo. Utabiri unaonesha chama kikuu cha upinzani Renamo huenda kikatwaa madaraka kwenye kiasi mikoa mitano kati ya hiyo 11. Rais Phillipe Nyusi jana wakati akipiga kura yake alisema huu ni uchaguzi unaofuatiliwa sana kuliko mwingine wowote nchini Msumbiji ,katika kanda hiyo na pengine Afrika kwa ujumla.

Wahlen in Mosambik
Picha: Getty Images/AFP/G. Guercia

Lakini mgombea urais kutoka  chama kikuu cha upinzani Renamo Ossufo Mamade alimtolea mwito Nyusi kukubali uwezekano wa kushindwa kwenye uchaguzi huu na kuwatia moyo wanamgambo wa chama chake kutohujumu uwazi katika mchakato huu.

Mgombea huyo wa Renamo anasema chama chake hakitokuwa tayari abadan,asilan  kukubali  matokeo ya uchaguzi ya udanganyifu na kuongeza kutowa onyo kwamba kuwanyima ushindi waliowengi  kuliipeleka nchi hiyo kwenye uhasama wa kijeshi katika miaka ya nyuma.Kiasi watu milioni 13 wamejiandikisha kupiga kura kati ya raia milioni 30 wa nchi hiyo. Shughuli ya kuhesabu kura imeanza na matokeo ya mwanzo yanatarajiwa kutangazwa kesho alhamisi.

Mwandishi:Saumu Mwasimba

Mhariri: Sekione Kitojo