1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchumi wa China kukua kwa asilimia 8

Sekione Kitojo5 Machi 2009

Waziri mkuu wa China Wen Jiabao amesema nchi yake itaongeza matumizi yake mwaka huu na kufikia lengo la ukuaji wa uchumi wa asilimia 8, lakini bila fedha zaidi kwa kichocheo cha uchumi.

https://p.dw.com/p/H653
Waziri mkuu wa China Wen Jiabao akisoma ripoti yake wakati wa ufunguzi wa kikao cha bunge la taifa mjini Beijing siku ya Alhamis.Picha: ap

Waziri mkuu Wen Jiabao amesema kuwa China itaongeza matumizi yake mwaka huu na kufikia lengo lake la ukuaji wa uchumi unaofikia asilimia 8 lakini haijatangaza ongezeko katika mpango wake mkubwa wa kichocheo cha uchumi wa miaka miwili kama inavyotakiwa na masoko ya hisa duniani.


Katika ripoti yake ya kila mwaka jana Alhamis katika bunge la wananchi wa China, , Wen amesema kuwa lengo la ukuaji wa uchumi kwa mwaka 2009 ni sahihi licha ya ongezeko la mzozo wa kiuchumi duniani. Iko haja ya kusisitiza kuwa kwa kupanga ukuaji wa pato jumla la taifa la asilimia 8, tumeangalia mahitaji yetu pamoja na uwezo wa hatua endelevu za maendeleo nchini China, amesema waziri mkuu Wen Jiabao.

Iwapo tutatumia sera sahihi pamoja na kuchukua hatua sahihi na kuzitekeleza kwa kina, tutaweza kufanikisha lengo hili.

Masoko ya hisa duniani yalipanda siku ya Jumatano kutokana na taarifa kuwa Wen ataongeza dola bilioni 585 katika mpango wa nchi hiyo wa kichocheo cha uchumi , mpango uliotangazwa hapo Novemba mwaka jana ili kupambana na hali ya inayoongezeka ya ukosefu wa nafasi za kazi hali ambayo inaweza kutishia amani katika jamii nchini humo kitu ambacho kinaenziwa na chama tawala cha kikomunist.

Ukuaji wa kiuchumi wa asilimia 8 unaangaliwa kuwa ni mahitaji ya wastani ili kuweza kuzuwia ukosefu wa kazi. Wen amesema kuwa nakisi katika bajeti ya China mwaka huu kinachofikia kiasi cha Yuan bilioni 950 katika sarafu ya China itapanda kwa hadi asilimia 3 na pato jumla la taifa kutoka asilimia 0.4 mwaka jana 2008.

Ikilinganishwa, Marekani inapanga kuwa na nakisi katika bajeti inayofikia kiasi cha asilimia 12.3 ya pato jumla la taifa mwaka huu.

Matumizi kwa ajili ya uwekezaji , katika kila sekta kuazia reli, hadi nyumba, yataongezeka maradufu , matumizi ya ziada katika huduma za afya yataongezeka kwa asilimia 38, na matumizi kwa ajili ya misaada ya kijamii pamoja na ajira yatapanda kwa asilimia 22, kwa mujibu wa bajeti ya mwaka 2009.

Lakini Wen ametangaza kuwa hakuna ongezeko katika mpango uliotangzwa Novemba mwaka jana katika hatua ya kuufufua uchumi mkubwa kabisa wa tatu duniani, ambao umeathirika na kupungua kwa mahitaji ya bidhaa zake za kuuza nje pamoja na kuporomoka kwa soko lake la hisa.

Wataalamu wa uchumi wanasema kuwa bado wanatarajia kuwa China itaongeza matumizi yake iwapo kutakuwa na mahitaji ya kufanya hivyo.

Ni dhahiri kuwa wanaangalia uchumi wa dunia ambao unayumba yumba siku hadi siku, kwa hiyo huenda wameamua kuzuwia kwanza matumizi zaidi, amesema Stephen Green , mkuu wa utafiti katika benki ya Standard Chartered mjini Shanghai.

Green amedokeza kuwa miradi ya kwanza itakarogharamiwa chini ya mpango huo wa kichocheo cha uchumi ndio kwanza inapatiwa fedha.

►◄


Sekione Kitojo/RTRE/AFPE