1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UEFA: Kashfa ya kupanga matokeo katika kandanda barani Ulaya.

Sekione Kitojo24 Novemba 2009

Wapelelezi nchini Ujerumani wamegundua kashfa kubwa ya kupanga matokeo katika michezo ya mpira wa miguu kuwahi kutokea katika historia ya mchezo huo barani Ulaya.

https://p.dw.com/p/KcIx
Rais wa shirikisho la kandanda nchini Ujerumani DFB ,Theo Zwanziger, DFB, kushoto na rais wa ligi ya Ujerumani.Picha: AP

BERLIN

Wapelelezi nchini Ujerumani wamegundua kashfa kubwa ya kupanga matokeo katika michezo  ya   mpira wa miguu kuwahi kutokea katika historia ya michezo barani Ulaya. Waendesha mashitaka wamesema kashfa hizo zimejitokeza katika michezo 200 za mpira wa miguu zilizochezwa mwaka huu katika ligi tisa za juu barani Ulaya, zikiwemo angalau michezo   mitatu ya Champions League.

Polisi nchini Ujerumani, Uingereza, Austria na Uswisi kwa ushirikiano wamewakamata watu kadhaa, 17 wakiwa ni kutoka Ujerumani na wawili Uswisi. Kiasi watuhumiwa wengine 200 wanachunguzwa kwa kuwahonga wachezaji, makocha, waamuzi  na maafisa wa vilabu.

Mkuu wa polisi katika mji wa Bochum, Ujerumani, Friedhelm Althans amesema kashfa hiyo huenda ikaongezeka zaidi. Ameongeza kuwa hongo hiyo inaweza kufikia euro milioni 10 ambazo ni sawa na dola za Marekani milioni 15.