1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ufaransa yataka kuepusha kugawika kwa taifa la CAR

Mjahida1 Machi 2014

Rais wa Ufaransa ameiambia Jamhuri ya Afrika ya Kati, wanajeshi wa Ufaransa walioko huko watafanyakazi kuiepusha nchi hiyo isigawike, na kuwapokonya silaha wanamgambo na makundi ya wahalifu wanaowapiga vita Waislamu.

https://p.dw.com/p/1BHpl
Rais wa Ufaransa Francois Hollande
Rais wa Ufaransa Francois HollandePicha: Reuters

Akiwasili mjini Bangui kutoka Nigeria, alikohudhuria sherehe ya miaka 100 ya muungano wa nchi hiyo, Rais Hollande alikutana na rais wa mpito wa Jamhuri ya Afrika ya kati Catherine Samba-Panza na pia kuwahutubia wanajeshi wa Ufaransa. Hii ni ziara ya pili ya Francois Hollande tangu mwezi Desemba mwaka jana na inakuja wakati kukiwa na ongezeko la wanajeshi wa kulinda amani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Siku ya Jumanne bunge la Ufaransa lilipiga kura kurefusha muda wa wanajeshi wa Ufaransa nchini humo, licha ya Wafaransa wenyewe kutounga mkono ushirikishwaji wa wanajeshi wao katika koloni lake hilo la zamani.

Wakati huo huo Umoja wa Mataifa umesema watu milioni moja wameikimbia nchi hiyo tangu kuanza kwa ghasia za kimadhehebu mwaka uliopita na kwamba watu wapatao milioni 1.3 wanahitaji msaada wa haraka wa chakula katika nchi hiyo ya Afrika.

Baadhi ya wanajeshi walioko Jamhuri ya Afrika ya Kati
Baadhi ya wanajeshi walioko Jamhuri ya Afrika ya KatiPicha: Issouf Sanogo/AFP/Getty Images

Miezi minne iliopita, Ufaransa ilituma wanajeshi wake ambao kwa sasa wamefikia takriban 2000 katika nchi hiyo ilio na idadi kubwa ya Wakristo, na waasi wa Kiislamu wa kundi la Seleka walichukua madaraka baada ya mapinduzi waliyofanya mwezi Machi mwaka Jana, na wamekuwa wakisukumwa nyuma na wanamgambo wa kundi la "anti-balaka."

Kando na kuwepo kwa wanajeshi wa Ufaransa, Wanajeshi 6000 wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika (MISCA) pia wapo nchini humo huku takriban wanajeshi 1000 wa Umoja wa Ulaya wakiwa bado wanatarajiwa kuwasili Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Samba Panza atoa wito wa kuundwa kikosi cha kulinda amani cha U.N

Hata hivyo akizungumza mjini Geneva, baada ya miezi miwili ya kusimamia shirika la Umoja wa Mataifa la ulinzi wa Raia mjini Bangui, Philippe Leclerc, amesema bado nchi hiyo haina wanajeshi wa kutosha wa kulinda amani.

Ulinzi mdogo ulililazimisha shirika hilo la Umoja wa Mataifa kuwahamisha baadhi ya raia.

Rais wa mpito Samba Panza
Rais wa mpito Samba PanzaPicha: Eric Feferberg/AFP/Getty Images

Rais wa mpito Samba-Panza mara kwa mara amekuwa akitoa wito wa kuundwa kwa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa nchini mwake. Katibu Mkuu wa Umoja huo Ban Ki-moon anatarajiwa kutoa ripoti wiki ijayo, ya kuangalia uwezekano wa kukibadilisha kikosi cha MISCA kuwa kikosi cha Umoja wa Mataifa. Netsanet Belay, Mkurugenzi wa utafiti na utetezi wa shirika la Amnesty International, amelitaka baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuridhia hatua hiyo mara moja.

Kwa upande mwengine madaktari wasio kuwa na mipaka (MSF) wamesema zaidi ya wakimbizi 8000 waliwasili kusini mwa nchi jirani ya Chad tangu mwishoni mwa mwezi wa January.

Hata hivyo kundi la antibalaka linasemekana linawafuata Waislamu kule wanakokwenda na kujaribu kuwashambulia wakati wakijaribu kukimbia ghasia.

Mwandishi: Amina Abubakar/Reuters

Mhariri: Sekione Kitojo