1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uhispania yaadhimisha siku ya kitaifa na mgogoro unaendelea

Zainab Aziz
12 Oktoba 2017

Maelfu ya Wakatalani waonataka Catalonia ibaki ndani ya Uhispania wameadhimisha siku ya kitaifa. Kitisho cha kujitenga kwa jimbo hilo kimeitumbukiza nchi hiyo kwenye sintofahamu. 

https://p.dw.com/p/2lkFp
Spanien Madrid Demonstration gegen Unabbhähigkeit Kataloniens
Picha: Getty Images/AFP/J. Soriano

Katika mji mkuu wa Madrid, vikosi vya jeshi na polisi vilisimama katikam gwaride mbele ya Mfalme Felipe VI, aliyekuwa ameongozana na wanasiasa wa kitaifa pamoja na wa mikoa. Maelfu ya watu waliokuwa wamejipanga katika njia ya Paseo de la Castellana ya mjini Madrid kwa ajili ya kushuhudia gwaride la kijeshi, walipeperusha bendera za Uhispania.

Uhispania inasubiri majibu kutokana na ombi la serikali kwakiongozi wa Catalonia Carles Puigdemont juu ya ufafanuzi iwapo tayari ametangaza uhuru. Ikiwa hivyo, serikali kuu ya Uhispania inaonya kuwa inaweza kutumia kifungu cha 155 cha katiba yake ili kuchukua udhibiti wa jimbo la Catalonia kwa sehemu au kwa ukamilifu.

Rais wa mkoa wa Catalonia Carles Puigdemont alitangaza siku ya Jumanne kwamba atautumia ushindi wa kura ya maoni  iliyopigwa marufuku kuendelea mbele na kutangaza uhuru wa jimbo la Catalonia na kisha akasimamisha uamuzi huo kwa kipindi cha wiki moja ili kupisha mazungumzo na fursa ya kuweza kupatana na serikali kuu ya mjini Madrid.Lakini akizungumza katika bunge la taifa, Waziri Mkuu Mariano Rajoy alisema majibu ya Puigdemont kutokana na matendo yake yatakuwa muhimu katika kuamua matukio katika siku zijazo.

National-Feiertag in Spanien
Mfalme Felipe wa VI na malkia LetiziaPicha: picture-alliance/AP Photo/P. White

Ni sikukuu gani hiyo?

Sikukuu ya leo nchini Uhispania  inajulikana kama Dia de la Hispanidad, kwa maana ya Siku ya Uhispania.  Nchi hiyo inakumbuka kuwasili nchini Marekani kwa Christopher Columbus na pia ni siku ya majeshi ya Uhispania. Viongozi wa Mikoa kwa kawaida hualikwa kuhudhuria gwaride mjini Madrid lakini kwa miaka mingi wawakilishi wa mikoa ya Basque na Catalonia wamesusa kuhudhuria maadhimisho hayo. Ofisi kadhaa za manispaa mjini Catalonia zimesema zitapuuza siku kuu hiyo na kuendelea kazi kama kawaida. Takriban raia milioni 2.3 wa Catalonia au asilimia 43 ya Wapiga kura katika jimbo hilo walipiga kura katika kura ya maoni ya kutafuta uhuru wa jimbo hilo. Asilimia 90 ya Wakatalonia waliunga mkono jimbo lao kujitenga na Uhispania.

Siku hiyo ilikumbwa na vurugu wakati polisi walipotumia nguvu pale walipojaribu kuzuia kufanyika kura hiyo ya maoni ambayo mahakama ilisema kuwa si halali. Ripoti ya shirika la Haki za Binadamu la Human Rights Watch iliyotolewa siku ya Alhamisi ilisema polisi wa Uhispania walitumia nguvu nyingi wakati wa kuwakabili waandamanaji waliokuwa wakiandamana kwa amani siku hiyo. 

Jimbo la Catalonia lina wakazi milioni 7.5 na linachangia asilimia 20 katika uchumi wa Uhispania unaofikia Euro trilioni 1.1 sawa na Dola trilioni 1.3.

Mwandishi: Zainab Aziz/APE

Mhariri: Mohammed Khelef