1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani kabla finali

26 Juni 2008

Ujerumani inacheza finali ya kombe la Ulaya jumapili hii mjini Vienna.Je, itatwaa kombe lake la 4 la Ulaya ?

https://p.dw.com/p/ERYC
Michael Ballack,nahodha wa Ujerumani.Picha: AP

Timu 2 ziitakazocheza finali jumapili hii ijayo mjini Vienna sasa zinajulikana baada ya kumalizika nusu-finali ya pili kati ya Spain na Russia .

Ujerumani ikiwa mabingwa mara 3 wa Ulaya na dunia, inapigiwa upatu itatawazwa kwa mara ya 4 mabingwa wa Ulaya.Hatahivyo, kuna wanaosema kocha wa Ujerumani, Joachim Loew, ana kazi kubwa bado ya kukiandaa kikosi chake kwa zahama ya jumapili.

►◄

Ujerumani,ilifanya kila kitu kinyume na mambo ilipocheza juzi na Uturuki katika changamoto yao ya nusu-finali ,lakini licha ya madhambi mengi katika ngome yake,iliondoka mwishoe, na ushindi wa mabao 3-2.Baada ya kujikuta waturuki wametangulia kutia bao kipindi cha kwanza,dakika chache walionesha ustadi wao wa kawaida na lango la Uturuki likatikisika pale Lukas Podolski alipomlishia tena dimba kama alivyofanya dhidi ya Ureno nae Schweinsteiger akasawazisha.Punde si punde, Miroslav Klose,mtiaji mabao mengi kabisa katika kombe lililopita la dunia 2006, akaongeza bao jengine kwa Ujerumani.

Lakini baada ya Uturuki kusawsazisha 2-2 huku zikisalia dakika 4 tu kabla firimbi ya mwisho kulia,ilionekana kana kwamba, watoto wa kocha wa Uturuki Fatih Terim,wanavuka tena salama usalimini na kutoroka tena na ushindi.

Wajerumani lakini walibainisha hata nao hawakati roho na mapema na sio kama Uswisi,jamhuri ya Czech wala Croatia.

Wajerumani kupitia Philipp Lahm,waliwatia kitanzi waturuki mara hii dakika ya 90 na ya mwisho ya mchezo.

Baadae kocha wa Ujerumani Joachim Loew alifungua mdomo na kudai "Tuna ari ya kushinda na sasa tunalitaka kombe."

Kwa kweli,Ujerumani nadra ilicheza dimba.Mara nyingi ikipiga mpira tu usoni ambao mara kwa mara waturuki wakiuzima.

Waturuki walicheza dimba licha ya kuwa wachezaji wao hadi 6 hawakuweza kucheza.Mpambano ule ulikua wazi -timu yoyote ingeliweza kushinda.

Itakapoteremka finali, Ujerumani itaonja ladha tofauti ya dimba.Adui yake keshokutwa anapenda kushambulia usoni,lakini sio kama inavyocheza Uturuki.

Chini ya kocha Loew,wajerumani hutamba zaidi wanaporejesha kwa kasi mashambulio kuliko wanapojenga mchezo kutoka kati ya uwanja.Hivyo, basi wakiregezewa kamba jumapili hii, hakuna ataeizuwia Ujerumani ikicheza hivyo, kuvaa taji la 4 la kombe la ulaya.

"Baada ya kufika hatua hii ya finali,bila shaka tunataka ushindi na tutaionesha ari yetu ya kushinda katika finali hii."-alisema kocha Joachim Loew.

Rais wa Shirikisho la dimba la Ujerumani,Theo Zwanziger, amemualika kocha wa zamani wa taifa katika kombe lililopita la dunia, Jürgen Klinsmann kuwa mgeni wa heshima jumapili hii mjini Vienna.Klinsmann kuanzia mwezi ujaoanakua kocha wa mabingwa Bayern Munich.

Kwa kuiingiza finali ,kila mchezaji wa Ujerumani ameahidiwa kitita cha Euro 150.000.Na wakiondoka na kombe je ?