1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaelezea wasiwasi kuhusu nyuklia

6 Januari 2021

Waziri wa Mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas amesema kuna "hatari kubwa" katika juhudi za ulimwengu za kupunguza matumizi ya silaha za nyuklia.

https://p.dw.com/p/3na4w
Heiko Maas
Picha: Getty Images/AFP/O. Andersen

Maas ameyasema hayo wakati akielekea Jordan leo hii Jumatano katika mkutano wa kimataifa utakaojadili swala la Nyuklia.

Akizungumza kabla ya kuanza safari yake kuelekea Jordan, waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas alisema katika miaka michache iliyopita "Udhibiti wa silaha duniani bado haujaimarika na badala yake umekuwa ukidhoofika kutokana na vishawishi tofauti na maendeleo.

Maas amesema hii ni dhahiri haswa katika swala la kutokomeza silaha za nyuklia ambalo analiona kuwa ni la hatari sana,na ameongeza kusema kwamba usalama wa bara la Ulaya unategemea kuondolewa kwa silaha za nyuklia na ulimwengu kuwa huru kutokana na silaha hizo. Soma Zaidi kudhibiti silaha za nuklia kuna matumaini gani ?

Waziri huyo atahudhiria mkutano wa tatu wa mawaziri utakaofanyika mjini Stocholm, Sweden. Mataifa 16 yataungana katika juhudi za kushinikiza kusitishwa matumizi ya silaha za Nyuklia. Soma zaidi Mkataba wa kupunguza silaha za nuklia

Wawakilishi wa mataifa 13 kati ya washiriki hao 16 watashiriki kwa njia ya video isipokuwa Waziri wa mambo ya Nje wa Ujerumani Heiko Maas, pamoja na waziri wa mambo ya nje wa Jordan na Sweden ambao watakutana ana kwa ana.

Schweden Ministertreffen zur nuklearen Abrüstung in Stockholm
Picha: Getty Images/AFP/C. Bresciani

Mikataba iliyopo

Kwa mujibu wa shirika la Habari la Petra la Jordan, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres  pia anatarajiwa kushiriki katika mkutano huo na kutoa hotuba.

Mkutano huo unajiri wiki moja kabla ya kuanza kwa makubaliano mapya kati ya Marekani na Urusi yaliyofikiwa juu ya kupunguza matumizi ya silaha za Nyuklia yatakayoanza rasmi mwezi Februari. Aidha mkataba wa Umoja wa Mataifa wa kusitisha matumizi ya silaha za Nyuklia utaanza kutumika mnamo Januari 22, ingawa mataifa yenye nguvu yanayomiliki nyuklia na nchi wanachama wa NATO hadi sasa wameukataa, wakisema kuwa mikataba iliyopo sasa inatosha. Soma zaidi Urusi na Marekani zasaini mkataba wa START

Deutschland Büchel | Greenpeace protestiert gegen Atomwaffen mit Heißluftballon
Picha: picture-alliance/dpa/T. Frey

Siku ya Jumatatu, licha ya juhudi za miaka mingi za Ulaya kuokoa mpango huo, Iran ilitangaza kuwa imeanza kuimarisha madini ya Uranium kwa asilimia 20, ikiwa ni nje ya kikomo cha asilimia 3.67 kilichowekwa katika makubaliano ya 2015 na mataifa 6 yenye nguvu kubwa za kiuchumi.

Safari ya kuelekea Jordan itakuwa ya kwanza kwa Heiko Maas katika kipindi cha miezi minne. Wawakilishi wengine wa mpango wa Stockholm ni pamoja na Arjentina, Ethiopia, Finland, Canada, Kazakhstan, Indonesia, Japan, New Zealand, Uholanzi, Norway, Switzerland, Uhispania na Korea Kusini.

/DPAE