1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulimwengu wamwombea Michael Schumacher

3 Januari 2014

Michael Schumacher alinuia kuadhimisha miaka 45 ya kuzaliwa kwake akiwa na jamaa na marafiki zake wa karibu, akiwa katika mapumziko ya msimu wa baridi nchini Ufaransa, lakini mambo hayakwenda hivyo.

https://p.dw.com/p/1Akxj
Schumacher-Fans zeigen Unterstützung für ihr Idol
Picha: Jean-Pierre Clatot/AFP/Getty Images

Siku tano baada ya kupata ajali mbaya wakati akishiriki mchezo wa kuteleza juu ya barafu, shujaa huyo aliyestaafu kutoka mbio za magari ya Formula One bado yuko katika hali mbaya hospitalini ijapokuwa madaktari wanasema wameidhibiti hali yake.

Ajali ya Schumacher imevigonga vichwa vya habari kote ulimwenguni, huku ujumbe ukiendelea kumiminika kutoka kila pembe wa kumtakia ahueni ya haraka. Schumacher bado yuko katika chumba cha wagonjwa mahututi.

Na kama hatua ya kuonyesha mshikamano na familia ya bingwa huyo wa Formula One, mashabiki wamekesha usiku kucha, wakimwombea Schumi. Kampuni aliyoihudumia ya Ferrari, iliwasafirisha mashabiki kwa mabasi kutoka Italia hadi mjini Grenoble, kusini mashariki ya Ufaransa, ili kumwombea shujaa wao. Nami hapa kwa niaba ya jamii ya DW tunajiunga na ulimwengu katika kumtakia shujaa huyo ahueni ya haraka.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman