1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa kuinusuru Sudan Kusini

30 Aprili 2014

Maafisa wakuu wa Umoja wa Mataifa leo wameapa watafanya kila wawezalo kuzuwiya Sudan Kusini kutumbukia katika mauaji ya halaiki na kuyaonya makundi yanayopingana yatawajibishwa iwapo baa la njaa litaibuka nchini humo.

https://p.dw.com/p/1Brhy
Kamishna Mkuu wa Haki za Binaadamu wa Umoja wa Mataifa Navi Pillay (kulia) mjumbe wa kuzuwiya mauaji ya halaiki Adama Dieng(katikati) wakikutana na kiongozi wa waasi Riek Machar (kushoto) Sudan Kusini.(29.04.2014)
Kamishna Mkuu wa Haki za Binaadamu wa Umoja wa Mataifa Navi Pillay (kulia) mjumbe wa kuzuwiya mauaji ya halaiki Adama Dieng(katikati) wakikutana na kiongozi wa waasi Riek Machar (kushoto) Sudan Kusini.(29.04.2014)Picha: picture-alliance/dpa

.Akiwashambulia vikali Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini na kiongozi wa waasi Riek Machar, Kamishna Mkuu wa Haki za Binaadamu wa Umoja wa Mataifa Navi Pillay amesema amefadhaishwa na kile kinachoonekana kuwa kutokuwepo kwa hofu juu ya hatari ya kuzuka baa la njaa nchini humo kulikoonyeshwa na viongozi hao wote wawili.

Kauli hiyo imekuja baada ya Pillay akiandamana na mjumbe maalum wa masuala ya mauaji ya halaiki kuwa na mazungumzo na viongozi hao hasimu ikiwa ni siku moja baada ya Umoja wa Mataifa kutowa wito wa dharura wa kusitishwa mapigano kwa mwezi mmoja kuepusha janga la njaa na maafa ya kibinaadamu.

Pillay amekaririwa akisema uwezekano wa kuzuka njaa nchini kote na utapia mlo utakaowaathiri mamia na maelfu ya watu wao kwa sababu ya kushindwa kwao binafsi kutatuwa tafauti zao kwa amani hakuonekani kuwapa wasi wasi mkubwa.

Kuzuwiya Rwanda nyengine Afrika

Mjumbe wa Umoja wa Mataifa wa kuzuwiya mauaji ya halaiki Adama Dieng amewaambia waandishi wa habari kwamba wanatakiwa waahidi kwa wahanga wa mauaji ya halaiki kuchukuwa hatua zote zinazowezekana wenye mamlaka nazo kuwalinda raia dhidi ya tukio jengine kama lile la Rwanda ambapo hakuna kisingizio cha kushindwa kuchukuwa hatua.

Msichana aliyepoteza makaazi akiwa katika kambi ya Umoja wa Mataifa kwenye eneo la Jebel kiunga cha Juba.
Msichana aliyepoteza makaazi akiwa katika kambi ya Umoja wa Mataifa kwenye eneo la Jebel kiunga cha Juba.Picha: picture-alliance/AP

Amesema katika mkutano na waandishi wa habari ambao pia umehudhuriwa na Pillay kwamba ni jambo la wazi kuwa mzozo huo umechukuwa mkondo wa hatari na raia wamekuwa wakishambuliwa kwa makusudi kwa misingi ya kikabila na uhusiano wao wa kisiasa.

Ziara hiyo ya Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini ambayo inamalizika leo hii inakuja wakati waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry akiwa ziarani barani Afrika ambapo pia anatazamiwa kuizuru Sudan Kusini.

Shinikizo kukomesha mapigano

Marekani ilikuwa mhusika mkuu katika kuisaidia Sudan Kusini kujipatia uhuru wake na Kerry ambaye awanasili Ethiopia leo hii kuanza ziara yake hiyo anatarajiwa kujaribu kuwashinikiza wasuluhishi katika mazungumzo ya amani yanayofanyika Ethiopia kukomesha mapigano hayo ya Sudan Kusini.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry.Picha: Reuters

Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya miezi minne nchini Sudan Kusini ambayo imejipatia uhuru wake kutoka Sudan hapo mwaka 2011 tayari vimesababisha kuuwawa kwa maelfu ya watu na wengine wanofikia mililoni moja nukta mbili wamelazimika kuyakimbia makaazi yao.

Makubaliano ya kusitisha mapigano yaliosainiwa mwezi wa Januari yako mashakani huku maelfu ya watu wakiwa wamepatia hifadhi kwenye makambi ya Umoja wa Mataifa kufuatia wimbi la mauaji ya kikabila ukiwemo ubakaji, kuwaingiza watoto jeshini kwa nguvu na kufanya mauaji kwenye mahospitali,kanisani na miskitini.

Mwandishi: Mohamed Dahman/AFP

Mhariri : Josephat Charo