Umoja wa Mataifa na Mashariki ya kati
4 Januari 2009
Baraza la usalama la umoja wa mataifa limeshindwa kwa mara nyengine tena kuafikiana juu ya msimamo wa aina moja unaobidi kufuatwa katika mzozo kati ya wa-Israel na wa-Palastina.Baada ya majadiliano ya saa nne,imetajwa kwamba wengi wa wanachama wanataka silaha ziwekwe chini haraka.Marekani lakini imepinga mswaada wa azimio ulioshauriwa na Libya,kwa hoja unalinganisha opereshini za kijeshi za Israel na harakati za kundi la kigaidi mfano wa Hamas.Hamas imechapisha ripoti inayokosoa kile walichokiita "Kiroja cha kushindwa baraza la usalama kufikia makubaliano ya kumaliza uhasama huko Gaza.Ujumbe wa Umoja wa Ulaya,ukiongozwa na waziri wa mambo ya nchi za nje wa jamhuri ya Tcheki,unaanza juhudi za upatanishi hii leo Mashariki ya kati, kwa lengo la kuwekwa chini silaha huko Gaza.Kituo cha kwanza cha ziara ya ujumbe huo ni Cairo nchini Misri,kesho ujumbe huo wa Umoja wa Ulaya utakua mjini Jerusalem kwa mazungumzo pamoja na viongozi wa Israel kuhusu mzozo wao pamoja na Hamas.Umoja wa Ulaya ndio wafadhili wakubwa wa wapalastina.