1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Mataifa wazitaka Kongo na Rwanda kuangaza mbele

11 Septemba 2012

Umoja wa Mataifa umeunga mkono juhudi za amani za marais wa nchi za Maziwa Makuu kwa ajili ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na kuitisha mkutano wa marais wa nchi hizo mwishoni mwa Septemba jijini New York.

https://p.dw.com/p/166d2
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Herve Ladsous
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Herve LadsousPicha: picture-alliance/Kyodo

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayehusika na Ulinzi wa Amani, Hervé Ladsous, na aliye ziarani nchini Kongo amesema kwamba viongozi wa Kongo na Rwanda ni lazima watizame mbele ili kuepusha kanda ya Maziwa Makuu kuingia tena kwenye vita.

Kwenye mkutano na wandishi habari hapa mjini Kinshasa,naibu katibu mkuu wa umoja wa mataifa anayehusika na ulinzi wa amani, Hervé Ladsous amesema kwamba raia wa Kivu wana haki ya kuishi kwa amani na kupewa hifadhi.

"Tunatakiwa kufanya kila kitu, ili mapigano yasitishwe na ili usalama uweze kurejea kwenye jimbo la Kivu. Mbali na hilo ni lazimat ufahamu kwamba kuna tatizo kuhusu mpaka wa Kongo ambayo inadai kuvamiwa na inaomba kutafuta suluhisho la tatizo hilo."

Ladous anaamini kwamba ili kupata suluhisho la kudumu baina ya Kongo na Rwanda ni lazima kuweko na mazungumzo kupitia mashirikiano ya kimkoa, mfano wa kongamano la nchi za Maziwa Makuu ama Jumuiya ya SADC au Umoja wa Afrika.

Wajibu wa Kongo uko mikononi mwa Waafrika wenyewe

Ladous amesema lengo la ziara yake nchini Kongo ni kujadiliana na viongozi wa Kongo kuhusu pendekezo la maraïs wa nchi za Maziwa Makuu ili kuwepo kwa kikosi cha kimataifa cha kuyasaka makundi ya waasi jimboni Kivu.

Vikosi vya serikali ya Kongo vinavyopambana na waasi wa M23.
Vikosi vya serikali ya Kongo vinavyopambana na waasi wa M23.Picha: Reuters

"Ni kwa Baraza la Umoja wa Mataifa kutoa uamzi wake kuhusu kikosi hicho cha kimataifa kwa ajili ya kuwasaka waasi. Kazi imekuwa ikifanyika ili kufikia hatua fulani, kwa sababu ni utashi wetu kurejea kwa amani kwenye neno hilo la Kongo. Na ni kwa sababu hiyo ndio tumefanya ziara hii."

Umoja wa Mataifa umeomba pendekezo la kuweko na kikosi cha kimataifa liweze kupewa ufumbuzi zaidi na maraïs wa nchi za Maziwa Makuu kabla ya Baraza la Usalama kuchukuwa hatua moja wapo katika uungwaji mkono wa kikosi hicho.

Ladsous amehimiza viongozi wa nchi za Maziwa Makuu kukuza amani baina yao ili kuepusha mizozo ya mara kwa mara.

"Kwa Raïs Paul Kagame (wa Rwanda) na kwa jumla ya viongozi wa kanda hili, ninaomba hasa na kabla ya yote kujenga imani baina yao. Na kupitia ushirikiano ambao sio wa pande mbili pekee bali wa kanda zima kuweko na juhudi za pamoja za kuweko na utulivu wa kanda hili la Maziwa Makuu."

Kuhusu madai ya kundi la M23 ya kwamba limealikwa pia huko New York, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema kwamba hafahamu lolote kuhusu mualiko huo.

Hapo jana Ladous alikuwa na mashauriano na waziri mkuu wa Kongo, Matata Ponyo, na baadhi ya mawaziri wengine akiwemo yule wa ulinzi. Leo anafanya mashauriano na Rais Joseph Kabila kabla ya kusafiri kwenda Goma. Ziara hiyo itampeleka hadi Kigali na Kampala.

Mwandishi: Saleh Mwanamilongo/DW Kinshasa
Mhariri: Mohammed Khelef