1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Ulaya kuijadili Uingereza na uhamiaji

17 Desemba 2015

Viongozi wa Umoja wa UIaya watayajadili masharti ya mageuzi yanayopendekezwa na Uingereza na suala la mgogoro wa wakimbizi katika mkutano wa kilele unaoandaliwa leo mjini Brussels

https://p.dw.com/p/1HOvh
Österreich Deutschland Flüchtlinge bei Passau
Picha: Reuters/M. Dalder

Changamoto hizo mbili zinatishia umoja wa jumuiya hiyo mnamo mwaka huu unaomalizika ambao umekuwa mojawapo ya vipindi vigumu kabisa katika historia yake.

Viongozi 28 wa Umoja wa UIaya kwanza wataujadili mpango wenye utata wa jeshi jipya la Umoja wa UIaya ambalo huenda likaweka doria katika mipaka bila idhini ya nchi mwenyeji, ili kudhibiti uhamiaji wakiwemo wakimbizi wanaotoka katika maeneo ya vita kama vile Syria.

Wakati wa chakula cha jioni mjini Brussels, Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron kisha atawasilisha masharti yake kwa mara ya kwanza kwa wenzake, akilenga kupata muafaka katika mkutano ujao wa kilele mwezi Februari ili kuepusha Uingereza kuondoka katika Umoja wa Ulaya kitu kinachofahamika maarufu kama “Brexit”.

Lakini mjadala huo unatarajiwa kuwa wa kishindo kwa sababu viongozi wengine 27 wa umoja huo inaaminika kuwa wanapinga kwa kauli moja sharti kuu la Uingereza ambalo ni kusubiri kwa miaka minne kabla ya wahamiaji wa Umoja wa Ulaya wanaofanya kazi Uingereza kuweza kupewa mafao yao.

EU-Gipfel / Brüssel
Mkutano wa Umoja wa Ulaya mjini BrusselsPicha: picture-alliance/dpa

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel, kiongozi mwenye nguvu kubwa barani Ulaya, alionya katika mkesha wa mkutano huo wa kilele kuwa suala la ujumuisho katika Umoja wa Ulaya halipaswi kujadiliwa, huku rais wa umoja huo Donald Tusk akisema “hakuna miiko” kuhusu suala hilo.

Mkutano huo wa kilele unahitimisha mwaka uliokuwa mgumu sana kwa Umoja wa Ulaya ambao umeufanya umoja huo kupambana na mkururo wa migogoro; – Ukraine, Ugiriki, uhamiaji, mashambulizi ya Paris na masharti ya Uingereza – ambayo yanatishia ndoto ya baada ya vita kuu ya dunia ya kuwa na bara lililoungana.

Mara nyingi, tatizo kuu limekuwa lile lile – fikra za kifedha na umoja wa kijiografia bila muundo wa kisiasa wa kuziunga mkono fikra hizo.

Wakati kukiwa na kuongezeka kwa vuguvugu la siasa za kizalendo na hofu kuwa mkataba wa Schengen wa Umoja wa UIaya unaoruhusu watu kutembea kwa uhuru kati ya nchi wanachama huenda ukavunjika, Umoja wa Ulaya uliogawika umeandaa msururu wa mikutano ya kilele ya dharura kuhusu mgogoro huo mwaka huu ili kutafuta ufumbuzi.

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wameiomba jumuiya hiyo kuweka ulinzi katika mipaka yake, kwa sababu ya mgogoro wa wahamiaji na pia kwa sababu za kiusalama hasa baada ya mashambulizi ya kigaidi ya Novemba mjini Paris.

Lakini mpango huo wa mpakani uliozinduliwa Jumatano, huenda ukasababisha mvutano katika mkutano wa leo wa kilele, huku Poland ikiutaja kuwa wa “kushangaza”.

Viongozi wanane wa Umoja wa UIaya kutoka kile kinachoitwa “muungano wa walio na nia” unaoogonzwa na Merkel wataandaa mkutano mdogo wa kilele na Waziri Mkuu wa Uturuki Ahmet Davutoglu kabla ya mkutano mkuu ili kujadili mpango wa kuwapa hifadhi wakimbizi moja kwa moja kutoka Uturuki.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Gakuba Daniel