1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Ulaya waidhinisha miongozo ya Brexit

29 Aprili 2017

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wameidhinisha masharti mazito ya talaka kwa Uingereza katika mkutano wa kilele Jumamosi (29.04.2017) na kuonyesha umoja wa aina yake wakati wa shida.

https://p.dw.com/p/2c8V1
Brüssel EU Gipfel Brexit Verhandlungen Merkel
Picha: Getty Images/AFP/E. Dunand

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wameidhinisha masharti mazito ya talaka kwa Uingereza katika mkutano wa kilele Jumamosi (29.04.2017) na kuonyesha umoja wa aina yake wakati wa shida lakini wakitambuwa fika huenda ugomvi ukaanza mara mazungumzo yatakapoanza.

Wakikutana kwa mara ya kwanza tokea Wazri Mkuu wa Uingereza Theresa May aanzishe rasmi kipengele cha kuanza kwa mazungumzo ya miaka miwili ya kujitowa kwa Uingereza katika Umoja wa Ulaya hapo nwishoni mwa Machi,viongozi wa mataifa 27 wanachama imewachukuwa dakika moja tu wakati wa chakula cha mchana kuidhinisha kurasa nane za miongozo  iliofikiwa na wanadiplomasia katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita.

"Miongozo imepitishwa kwa kauli moja.Mataifa 27 ya Umoja wa Ulaya na mamlaka yenye kuzingatia haki kwa ajili ya mazungumzo ya Brexit iko tayari." mwenyekiti wa mkutano huo wa kilele Donald Tusk ameandika kwenye mtandao wake wa Twitter.Maafisa wamesema viongozi wameshangilia baada ya kupitisha bila ya marekebisho rasimu iliyotayarishwa kwa kuzingatia mawazo yao.

Miongozo ya Brexit

Brüssel EU Gipfel Brexit Verhandlungen Tusk
Mwenyekiti wa Mkutano wa Kilele Donald Tusk.Picha: picture-alliance/dpa/M. Meissner

Miongozo hiyo itamuelekeza Michel Barnier mjumbe mkuu wa mazungumzo kwa upande wa Umoja wa Ulaya kutafuta makubaliano ambayo yatahakikisha kupatikana kwa haki kwa wataalamu milioni tatu wa Umoja wa Ulaya wanaoishi nchini Uingereza, kuhakikisha Uingereza inalipa mabilioni ya euro ambazo Umoja wa Ulaya inafikiri itakuwa inaidai nchi hiyo na kuepuka kuyumbisha amani kwa kuanzisha uvukaji mgumu wa mpaka kati ya Umoja wa Ulaya na Uingereza kwa kupitia kisiwa cha Ireland.

Barnier amesema "tuko tayari,tuko pamoja."Pia wamefuta uwezekano wa kujadili makabuliano ya biashara ambayo May anayataka hadi hapo watakapokuwa wameona kuna maendeleo juu ya masharti hayo makuu waliyokubaliana ya kujitowa kwa Uingereza.

"Kabla ya kujadili mustakbali,inabidi tutatuwe kile kilichosibu kipindi chetu kilechopita" amesema Tusk kauli ambayo pia imeshadidiwa na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani.

Kama ishara ya kutiliwa mashaka kwa umoja wenyewe wa Uingreza wakati wa kujitowa kwake viongozi pia watatowa ahadi kwa Waziri Mkuu wa Ireland Enda Kenny kwamba iwapo Ireland Kaskazini ambayo imepiga kura ya kupinga kujitowa kwa Uingereza ikitaka moja kwa moja itakuwa nchi mwanachama wa Umoja wa Ulaya.

Uingereza isionekane kufaidika

Brüssel EU Gipfel Brexit Verhandlungen
Mkutano wa Kilele wa Umoja wa Ulaya mjini Brussels.Picha: Reuters/V. Mayo

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wanaona kuwa ni muhimu isionekane kwamba Uingereza inafaidika na Brexit ili kuzuwiya nchi nyengine zisifuate mfano wake.

Maafisa waandamizi katika makao makuu ya Umoja wa Ulaya yalioko Brussels wanaamini hatari ya kuvunjika kwa mazungumzo ambako kunaweza kuiona Uingereza ikitoka tu kwa urahisi kwenye mkwamo wa vurugu wa kisheria kufikia Machi 2019 kumepunguwa tokea May amuandikie Tusk hapo mwezi wa Machi 29 kuhusiana na haja ya kufikia muafaka.

Kansela Merkel ambaye yeye mwenyewe anakabiliwa na uchaguzi nchini mwake hapo mwezi wa Septemba ameionya Uingereza wiki iliopita dhidi ya kuendekeza njozi juu ya kiasi cha nafasi itakazopata katika masoko ya umoja wa Ulaya.

Baadhi ya wanadiplomasia wanahofu madai ya Umoja wa Ulaya

yanaonekana kama ni makali mno na yanaweza kusababisha umma ukayagomea nchini Uingereza na kufaya iwe vigumu kwa May kufikia makubaliano.

Mwandishi : Mohamed Dahman/Reuters

Mhariri : Yusra Buwayhid