1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UNHCR yakiri udhaifu katika kushughulikia wakimbizi

Bruce Amani
20 Juni 2019

Kamishna mkuu  wa shirika la Umoja wa Mataifa linalowashughulikia wakimbizi UNHCR  Filippo Grandi ameliambia shirika la habari la DW kwamba kumekuwa na udhaifu katika kushughulikia idadi kubwa ya wakimbizi. 

https://p.dw.com/p/3KkmX
Äthiopien | Mehr als 200 Somalis sind in Zalanbessa von Tigray gestrandet, nachdem sie gezwungen wurden, Eritrea zu verlassen
Wakimbizi kutoka Somalia Picha: DW/M. Haileselassie

Fillipo Grandi amesema kuwa  shirika la UNHCR limefichua  kwamba idadi kubwa ya watu walilazimika kuyakimbia  makazi yao mwaka jana kwasababu ya vita na mateso. Mnamo mwaka 2018, takriban watu milioni 71 walipoteza makazi yao.

Akizungumza  na shirika hili la habari la DW kabla ya siku ya kimataifa ya wakimbizi, Kamishna huyo wa UNHCR alisema, kumekuwa na udhaifu mkubwa katika kushughulikia  idadi kubwa ya wakimbizi. Aliongeza kuwa wametambua kuwa bara la Ulaya kwa mfano limejipanga kwa idadi ndogo tu ya wakimbizi na kwamba idadi ya wakimbizi ilipoongezeka mwaka 2015, bara hilo halikuwa tayari na hivyo kutuma ujumbe usiofaa.

Filippo Grandi aliwashtumu baadhi ya wanasiasa ambao wametumia hali hiyo vibaya na kwamba wametambua kuwa kwa kuwaonyesha watu hawa kuwa tishio watapata uungwaji mkono na kura. Aliongeza kuwa hii ni mbinu isiyostahili ya kulishughulikia suala hili na haitatui tatizo lililoko.

Schweiz, Genf: UN-Beauftragte für Flüchtlinge Grandi und der UN-Koordinator für humanitäre Hilfe, Lowcock, nehmen an einer Pressekonferenz teil
Kamishna wa shirika la UNHCR- Fillipo GrandiPicha: Reuters/D. Balibouse

Baadaye alikiri kwamba kile kinachomtatiza ni hali hii ya mazingira iliyo na ubaguzi, shutuma na inayowaona wakimbizi, wahamiaji na wakati mwingine raia wa kigeni kuwa adui. Ni mtazamo ambao wengi wanazingatia kwasababu ya hofu, lakini haipaswi kuwa hivyo..

Grandi pia alizikosoa serikali zinazowafungia mipaka wakimbizi na wahamiaji.

Licha ya idadi kubwa ya watu waliopoteza makazi kote ulimwenguni, kamishna huyo wa shirika hilo la Umoja wa Mataifa linalowashughulikia wakimbizi amesema  hali hiyo bado inaweza kushughulikiwa . Alitolea mfano  ufanisi wa Uganda ambayo imepokea mamilioni ya wakimbizi kutoka Sudan Kusini na Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo.

Grandi amesema kuwa Uganda haina raslimali zote kwa hivyo ukarimu huo haupaswi kupuuzwa na kwamba inapaswa kusaidiwa. Aliongeza kuwa kwa kuiga mfano huo ambao kwasasa unatekelezwa katika takriban mataifa 15, kuna muongozo mpya kwa kusaidia kwa njia bora zaidi mzozo huo wa wakimbizi.