1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Union Berlin yamtema Sebastian Polter

Josephat Charo
28 Mei 2020

Union Berlin imesema Alhamisi (28.05.2020) mshambuliaji Sebastian Polter hataichezea tena klabu hiyo kabla mkataba wake kukamilisha mwishoni mwa msimu huu kutokana na "tabia ya kutotoa ushirikiano."

https://p.dw.com/p/3cv8u
Fußball Bundesliga 1. FC Union Berlin
Picha: Getty Images/Bongarts/A. Hassensteiner

"Ni mojawapo ya maadili msingi ya Union Berlin kwambba sisi kama klabu tunaunda jamii imara ambapo tunasimama pamoja kwa ajili ya kila mmoja na kwa ajili ya klabu," alisema rais wa Union Berlin Dirk Zingler.

"Sebastian, mchezaji pekee katika kikosi cha kwanza, timu ya makocha na kikosi cha akiba, kwa bahati mbaya hafanyi hivyo. Ni jukumu langu la mara moja, wakati huu mgumu, kuulinda umoja na mshikamano wa wafanyakazi wa klabu na kikosi kizima, ili tusihatarishe malengo yetu."

Taarifa za kina hazikutolewa na klabu ya Union Berlin lakini kwa mujibu wa taarifa za shirika la habari la Ujerumani dpa Polter hakutaka kujiunga na juhudi ya pamoja kuwalinda wafanyakazi wa klabu walioathiriwa kifedha na janga la virusi vya corona.

Polter, mwenye umri wa miaka 29, alijiunga na Union Berlin Januari 2017 na kuisaidia timu hiyo kufuzu kucheza katika ligi kuu ya Bundesliga kwa mara ya kwanza katika historia yake. Mkwaju wake wa penalti pia uliisaidia Union Berlin kushinda 1-0 dhidi ya watani wao wa mtaani Hertha Berlin mwanzoni mwa msimu.

Klabu ya Union Berlin imesema Polter ataendelea kufanya mazoezi na kikosi cha kwanza cha klabu hiyo.

(dpa)