1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi yatoka sare na Korea Kusini

18 Juni 2014

Alexander Kerzhakov alifunga goli mara tu baada ya kuingia uwanjani kama nguvu mpya na kuisaidia Urusi kutoka sare ya 1-1 na Korea Kusini. Mchuano huo uligubikwa na kosa la kwanza kubwa lililofanywa na mlinda lango

https://p.dw.com/p/1CKqM
FIFA Fußball WM 2014 Südkorea Russland Kerzhakov
Picha: Getty Images

Kipa wa Urusi Igor Akinfeev alitema ndani ya wavu wake shuti kali iliyovurumishwa kwa mbali na mchezaji Lee Keun-ho na kuizawadia Korea Kusini goli katika dakika ya 68 ya mchezo wa kundi H katika uwanja wa Arena Pantanal mjini Cuiaba.

Lakini nguvu mpya Kerzhakov alimkomboa mwenzake, kwa kufunga goli la kusawazisha katika dakika ya 74 baada ya kuingia uwanjani kuokoa jahazi lililokuwa likizama.

Akinfeev alikaa kitako ndani ya lango lake, mikono kichwani, baada ya kufanya kosa hilo, akiwa amefedheheka kwa kuangusha mpira kutokana na shuti ya umbali wa mita 30. Alitulizwa na wachezaji wenzake kadhaa, na dakika chache baadaye wakaungana katika kushangilia goli la kusawazisha.

Timu hizo mbili ziko nyuma ya Ubelgiji na pointi moja kila mmoja, baada ya Ubelgiji kuizaba Algeria magoli mawili kwa moja. Lakini kundi hilo linaonekana kuwa wazi kabisa ukizingatia matokeo ya mechi mbili za mwanzo.

Mwandishi: Bruce Amani/DW
Mhariri: Abdul-Rahman