1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi na china zinaingia katika Jamhuri ya Afrika ya Kati

Shisia Wasilwa
24 Mei 2018

Mataifa ya Urusi na china yanaingia kwa nguvu katika Jamhuri ya Afrika ya Kati huku ushawishi wa Ulaya katika taifa hilo lenye utajiri mkubwa wa madini na kieneo ukiendelea kupungua kwa mujibu wa wachambuzi.

https://p.dw.com/p/2yGeC
Militär Kongo
Picha: picture-alliance/ZUMAPRESS/D. Honl

Umoja wa Mataifa umeliweka taifa hilo katika nafasi ya miwsho kwenye nchi 188 zilizotajwa katika faharasi ya maendeleo ya kibinadamu huku mizozo ikishuhudiwa. Sehemu kubwa ya taifa hilo liko kwenye himaya ya waasi.

Sehemu kubwa ya nchi hiyo iko mikononi mwa makundi ya wanamgambo na vurugu zimesababisha robo ya wakaazi wake  milioni 4.5  kuyakimbia makaazi yao. Pamoja na kuonekana kuwa taifa masikini kuna utajiri mkubwa uliotapakaa kuanzia madini ya almasi na dhabu hadi shaba na Urani ambayo yanapatikana katika maeneo mengi ya nchi hiyo. Ufaransa koloni la zamani la nchi hiyo ndiyo nchi tangu jadi ikiyaingia masuala ya Jamhuri ya Afrika ya kati. Iliingia kijeshi mwaka 2013 baada ya kiongozi wa muda mrefu Francois Bozize kuondolewa kwa nguvu madarakani na kundi la waasi linalojumuisha zaidi waislamu la Seleka.

Ushawishi wa Ulaya unapungua 

Vikosi vya Umoja wa Mataifa vya kudumisha amani
Vikosi vya Umoja wa Mataifa vya kudumisha amaniPicha: picture-alliance/AA/H. C. Serefio

Ufaransa ikayakabidhi mamlaka ya kusimamia amani kwa ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa lakini idadi ya wanajeshi wake imepungua nchini humo hadi 81 ambao wanatowa mafunzo ya kijeshi pamoja na ndege zisizoendeshwa na rubani. Mwanzoni mwa mwezi huu Ufaransa ilipeleka ndege za kivita 2000 kutoka chad kupiga doria katika eneo zima la kaskazini kama hatua ya kutoa onyo kwa waasi wapiganaji wanaolidhibiti eneo hilo.

Wachambuzi wanasema kwamba matukio ya hivi karibuni yanaonesha msisitizo wa kuongezeka maslahi ya China na Urusi katika sehemu hiyo ambayo kwa kiasi kikubwa haishughulikiwi na ulimwengu. Afisa mmoja kutoka Umoja wa Mataifa mjini Bangui anasema Jamhuri ya Afrika ya Kati ni uwanja wa siasa za kieneo na kila mmoja anawania kupata fursa ya kuvutia kwake amesema afisa huyo ambaye hakutaka kutajwa jina. Anasema kwamba nchi moja inapoingia nchini humo nchi nyingine nazo zinafuatilia na kuchukua hatua mwafaka.

 Urusi iliichukua hatua kubwa mwishoni mwa mwaka uliopita wakati iliporuhusiwa na Umoja wa Mataifa kuipelekea Jamhuri ya Afrika ya katzi silaha na wanajeshi. Hatua hiyo ilikusudiwa kuipa nguvu serikali kuu pamoja na jeshi lake lililodhoofika na kuiondolea vikwazo vya silaha vilivyowekwa na Umoja huo mwaka 2013 wakati nchi hiyo ilipotumbukia kikamilifu katika vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Uingereza Ufaransa na Marekani zilizungumzia wasiwasi wao kuhusiana na hatua hiyo ya Urusi wakitaka silaha zilizokuwa zikipelekwa ziwe ni silaha ndogondogo na kwamba Urusi ichukue hatua za kufuatia zinakopelkwa silaha hizo ili kuzuia biashara ya silaha katika soko la biashara za magendo.

Urusi imesaini mikataba kadhaa 

Kwa hivi sasa inaaminika kwamba Urusi imesaini mikataba kadhaa ya kibiashara na serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati ambapo inatowa ulinzi kwa rais Fausitin Archenge Toudera, na makundi kadhaa ya wanamgambo yanasema yameshawahi kufuatwa na maafisa wa Urusi wakitaka kuwa wasuluhishi wa migogoro ya nchi hiyo.

Hali ya wasiwasi Jamhuri ya Afrika ya Kati
Hali ya wasiwasi Jamhuri ya Afrika ya Kati Picha: picture-alliance/AP Photo/A. Medichini

Kwa mujibu wa mwanadiplomasia mmoja kutoka nchi za Magharibi katika Umoja wa Mataifa, "nchi hizo za Magharibi zimeshapigwa kikumbo na sasa Warusi wako kila mahala katika vyombo vya dola nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati."

Inatajwa kwamba msafara wa kiasi malori 20 wa warusi ulibvuka na kuingia kaskazini mwa Jamhuri ya Afrika ya kati mwezi uliopita kutoka Sudan katika kile ambacho kinaelezwa na serikali ya Jamhuri ya Afrika ya kati kwamba ni ujumbe wa kusaidia ujenzi mpya wa hospitali zilizoharibika.

Rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Faustin Archange Toudera jumatano wiki hii aliwasili Urusi kuhudhuria mkutano wa kiuchumi unaofanyika Saint Petersburg ambako huenda akakutana na rais Putin.

Wachamabuzi wa kisiasa wanasema kwa kiasi kikubwa mabadiliko makubwa katika uhusiano wa nchi za Magharibi na Bara la Afrika ambapo zaidi nchi za Magharibi zimejikita zaidi katika uhusiano juu ya suala la wahamiaji na usalama. China ambayo inamwaga fedha Afrika nayo imejiingiza Jamhuri ya Afrika ya Kati ikitowa msaada wa kiuchumi kama ambavyo inafanya pia katika nchi nyingine za bara hilo.

Kwa hali kama hiyo mchambuzi Thierry Vircoulon, ambaye ni mtaalamu wa masuala ya Jamhuri ya Afrika ya kati kutoka taasisi ya ufaransa ya uhusiano wa kimataifa anasema Jamhuri ya Afrika ya kati anasema, "sasa hiyo ni nchi iliyopiga magoti,au kwa maneno mengine ni nchi inayouzwa. Wanunuzi ni nchi zinazoinukia kuwa na nguvu kubwa duniani kama China na nchi yenye nguvu tangu zamani Urusi hapa ikionekana katika harakati za kujikita upya na nchi za Magharibi sio tena wanunuzi."

Mwandishi: Shisia Wasilwa, Afp

Mhariri: Yusuf Saumu