1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uturuki yaishitaki Marekani WTO

Isaac Gamba
21 Agosti 2018

 Uturuki imewasilisha malalamiko katika shirika la biashara la kimataifa duniani (WTO) dhidi ya hatua ya Marekani kuongeza ushuru kwa bidhaa za chuma cha pua pamoja na bati zinazotoka Uturuki.

https://p.dw.com/p/33SmW
Schweiz | Hauptgebäude der WTO in Genf
Picha: picture-alliance/dpa/Xinhua/X. Jinquan

August 10 mwaka huu rais wa Marekani Donald Trump alitangaza kuwa ataongeza mara mbili  viwango vya kodi kwa asilimia 50 kwa bidhaa za chuma cha pua kutoka Uturuki na bati kwa asilimia 20 kufuatia mvutano unaoendelea  kati ya nchi hizo mbili unaomhusu mchungaji wa Marekani  Andrew Brunson anayeshitakiwa Uturuki kwa makosa kadhaa ukiwemo ugaidi.

Katika barua yake kwa WTO  Uturuki inadai  Marekani ilivunja sheria za biashara wakati ilipotangaza mwezi Juni kutoza  kodi kwa asilimia 25  bidhaa za chuma cha pua na bati asilimia 10 kwa nchi nyingi isipokuwa Argentina na Australia pekee.

 Kwa mujibu wa Uturuki hatua ya hivi karibuni ya Marekani dhidi ya Uturuki inazidiasha  ukiukaji huo wa sheria za WTO.

Wiki iliyopita Uturuki ilitangaza kujibu hatua hiyo ya Marekani kwa kupandisha kodi kwa bidhaa 22 tofauti za Marekani ikiwa ni pamoja na magari, mchele , vipodozi na tumbaku.

Chini ya sheria za  WTO  Uturuki na Marekani  sasa zinasiku 60 kumaliza mvutano huo kwa njia ya mazungumzo na kama zitashindwa kufikia muafaka basi shirika hilo litalazimika kutoa uamuzi.

 

Mchungaji Brunson chanzo cha mvutano

Andrew Brunson
Andrew Brunson Mchungaji kutoka MarekaniPicha: Reuters/Depo Photos

Mvutano kati ya Uturuki na Marekani umeongezeka kufuatia kuendelea kushikiliwa gerezani mchungaji wa Marekani Andrew Brunson nchini Uturuki  huku pia nchi zote zikitangaziana vikwazo kwa mawaziri wa pande zote mbili. Hata hivyo Brunson amekuwa akikanusha tuhuma dhidi yake.

Vikwazo vya Marekani dhidi ya Uturuki vimesababasha kuporomoka kwa sarafu ya Lira  ya nchi hiyo hali ambayo pia inaleta wasiwasi kwa mabenki ya ulaya kutokana na baadhi ya mabenki hayo kuwa na hisa katika  taasisi za kifedha nchini Uturuki.

Mchungaji Brunson anayetokea North Carolina ambaye ni chimbuko la mzozo wa sasa kati ya nchi hizo washirika wa NATO  uliosababisha pia  kuathirika kwa masoko ya kifedha nchini Uturuki  ameishi Uturuki kwa miongo miwili hadi sasa.

Ijumaa iliyopita rais Donald Trump wa Marekani akizungumza na waandishi wa habari  alisema kwa maoni yake anaona kuwa Uturuki wamefanya vibaya kuendelea kumshikilia Brunson kwani walipaswa kumuachia  muda mrefu uliopita.

Ameongeza kuwa hawako tayari kukaa kimya  wakati Uturuki inaendelea kumshikilia raia wake.

Ijumaa iliyopita mahakama  ya Uturuki ililikikataa ombi la kutaka kumuachia mchungaji Brunson anayezuiliwa katika kifungo cha nyumbani .

Mwandishi: Isaac Gamba/RTRE/DPAE

Mhariri    : Mohammed Abdul-Rahman