1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wagawika kuhusu bajeti

Sekione Kitojo
24 Februari 2018

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wamegawika katika mkutano wao mjini Brussels jana Ijumaa(23.02.2018)kuhusiana na wito wa kuchangia  zaidi kuziba pengo kubwa katika bajeti baada ya Uingereza kujitoa rasmi katika Umoja huo.

https://p.dw.com/p/2tG4d
EU Gipfel Plenum
Picha: Getty Images/AFP/L. Marin

Rais wa Umoja wa Ulaya Donald Tusk amesema  viongozi  ho  wa mataifa  27, wanaokutana  bila  ya  Uingereza  kujadili  mipango ya baadaye , wanataka  kuchangia zaidi  kuhusu  ulinzi, uhamiaji  na usalama.

Lakini hawakuafikia  juu  ya  iwapo  nchi  hizo zitalipia katika  bajeti ya  pamoja  kuziba  pengo  linaloachwa  wazi baada  ya  Uingereza kujitoa  kutoka  Umoja  huo yaani  Brexit la euro bilioni 15 kwa mwaka.

EU Gipfel Bettel, Merkel und Kurz
Waziri mkuu wa Luxembourg Xavier Bettel (kushoto) kansela wa Ujerumani Angela Merkel (katikati) na kansela wa Austria sebastian Kurz(kushoto) katika mkutano wa EU mjini Brussels.Picha: Reuters/Y. Herman

"Nchi  nyingi ziko  tayari  kuchangia  zaidi katika  bajeti  hiyo  ya kabla  ya  mwaka  2020," Tusk  aliwaambia  waandishi  habari, na kuongeza  kwamba  "wanahitaji kutatua  suala  hilo  la  pengo  la bajeti linalosababishwa  na  Brexit".

Mkuu wa  halmashauri ya Umoja  wa  Ulaya  Jean-Claude Juncker amesema  mataifa  14 ama  15 yamekubali kuongeza  mchango  wao wa  taifa, hali  ambayo  bado inaacha  karibu  nusu  ya  mataifa  ya kundi  hilo bado  hayajaamua  ama  kupinga.

"Mjadala haukuwa wa malumbano zaidi  kama nilivyotarajia," amesema  Juncker , akionya  hata  hivyo  kuwa :"Iwapo hakuna fedha  nyumbani mapenzi yanapeperuka nje  ya  mlango." Nchi muhimu  kiuchumi  kama  Ujerumani, Uhispania  na  Ufaransa ziko tayari  kulipa zaidi.

Upanuzi wa bajeti

Rais  wa  Ufaransa Emmanuel Macron  aliwaambia  waandishi habari kuwa Ufaransa iko tayari kupanua bajeti yake. Waziri  mkuu wa  uhispania Mariano Rajoy aliongeza: "nafikiri Uhispania inapaswa  kuwa  wazi  na  kutumbukiza  rasilmali  nyingi  zaidi." Lakini upinzani  unaongozwa  na  Uholanzi, Denmark, Sweden na Austria, nchi  ambazo  ni "wachangia wakubwa" ambao  wanalipa zaidi  katika  bajeti  ya  Umoja  wa  Ulaya  kuliko  zinavyopata.

EU Gipfel Merkel mit Tsipras und Borisow
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel(katikati) akizungumza na waziri mkuu wa Ugiriki Alexis Tsipras(kushoto) na waziri mkuu wa Bulgaria Boyko Boris(kulia)Picha: Reuters/Y. Herman

"Kile  tusichokitaka  ni  mzigo  wa  ongezeko  la  kila  mara  katika matumizi," Kansela  wa  Austria Sebastian Kurz  alisema.

Wakati huo  huo, Umoja  huo  umetoa kwa  baadhi  ya  mataifa  sita ya  eneo  la  Balkan  ambayo  yana  matumaini  ya  kujiunga  na kundi  hilo  la  mataifa  uwezekano wa  kuwa  wanachama  ifikapo mwaka  2025, lakini umezionya  nchi  hizo kwamba  bado  zina vikwazo  vya  kuvuka.

Mwongozo wa  halmashauri  ya  Umoja  wa  Ulaya  kwa  ajili  ya eneo  hilo uliowasilishwa  mapema  mwezi  huu unasena  nchi  hizo ni  lazima ziondoe matatizo yanayohusiana  na  rushwa na  utawala wa  sheria na  hususan kutatua  mizozo  kadhaa  inayotokota ya mipaka.

Mlango uko wazi

Mlango  wa  Umoja  wa  Ulaya  uko  wazi  kwa kuwaingiza  pale tu , nchi  moja  moja  zitakapotimiza  masharti ," mpango  huo  umesema.

EU Gipfel Juncker und Macron
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron (kushoto) akizungumza na rais wa halmashauri ya Umoja wa Ulaya Jean-Claude Juncker(aliyekaa)Picha: Reuters/Y. Herman

Mkuu  wa  halmashauri  ya  Umoja  wa  Ulaya Jean-Claude Juncker ataanza  zira  ya  eneo  hilo kesho  Jumapili kujadili mkakati  mpya, ambao  unasisitiza "utekelezaji wa mageuzi ya  msingi  pamoja  na mahusiano mazuri ya  ujirani".

Montenegro  na  Serbia ni  nchi  zilizoko  mbele  kujiunga pamoja  na Albania, Bosnia , Kosovo na  Macedonia zikiwa  nyuma, lakini  zote zinaingiwa  na  wasiwasi  baada  ya  Umoja  wa  Ulaya  kuzuwia upanuzi miaka  minne  iliyopita.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Caro Robi