1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi waanza kuwasili kwa mkutano wa G8

Charo, Josephat6 Julai 2008

Rais Bush aahidi kutoa mawazo ya kupunguza gesi ya carbon inayosababisha mabadiliko ya hali ya hewa

https://p.dw.com/p/EXBe
Rais wa Marekani George W. Bush (kushoto) na waziri mkuu wa Japan Yasuo Fukuda mjini ToyakoPicha: AP

Rais George W Bush wa Marekani amekutana leo mjini Toyako na waziri mkuu wa Japan Yasuo Fukuda huku viongozi wa nchi nane zilizoendelea kiviwanda duniani, G8, wakijiandaa kuanza mkutano wao wa kilele hapo kesho.

Mkutano huo wa siku tatu utakaofanyika mjini Toyako katika kisiwa cha Hokkaido kaskazini mwa Japan, utajadili uchumi wa dunia, mabadiliko ya hali ya hewa, maendeleo barani Afrika, mzozo nchini Zimbabwe, mzozo wa nyuklia wa Korea Kaskzini na mpango wa nyuklia wa Iran.

Alipokutana na waziri mkuu wa Japan Yasuo Fukuda hii leo, rais Bush ameahidi kwamba Marekani itachukua jukumu kubwa katika kupunuza gesi ya carbon kutoka viwandani ambayo inalaumiwa kwa kusababisha mabadiliko ya hali ya hewa.

Hata hivyo kiongozi huyo wa Marekani ameonya kuwa juhudi hizo hazitafaulu ikiwa China na India hazitahusishwa. ``Nitatoa maoni yatakayosaidia, lakini hatutafaulu kulitatua tatizo hili mpaka nchi mbili zinazoinukia kwa haraka kiuchumi, yaani China na India, zishiriki katika makubaliano yoyote ya muda mrefu.´´

Fukuda kuhudhuria michezo ya Olimpiki

Wakati wa mkutano na waandishi wa habari hii leo waziri mkuu wa Japan Yasuo Fukuda amesema atahudhuria sherehe za ufunguzi wa michezo ya Olimpiki itakayofanyika mjini Beijing nchini China akisema ni tukio kubwa la michezo na wala sio la kisiasa. Ameongeza kuwa ingawa China inakabiliwa na matatizo mbali mbali hakuna haja ya kuingiza siasa katika michezo ya Olimpiki.

Maandamano yafanyika

Mamia ya wanaharakati wamefanya maandamano kwa siku ya pili mfululizo mjini Sapporo, mji mkubwa uliokaribu na eneo la mkutano wa G8, wakilalamikia haki za wafanyakazi, mzozo wa Tibet na umaskini duniani.

Zaidi ya maafisa wa polisi elfu 20 wanashika doria katika kisiwa cha Hokkaido kutakakofanyika mkutano huo wa nchi za G8.