1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wahaha kujiengua kashfa ya Pandora

Lilian Mtono
4 Oktoba 2021

Baada ya ufichuzi wa viongozi mbalimbali kuficha mali nje ya nchi ili kukwepa kodi, viongozi hao wameibuka kuipinga vikali wengine wakisema ni uongo mtupu na isiyoaminika.

https://p.dw.com/p/41FJ9
König Abdullah II. von Jordanien | Porträt
Picha: Ameer Al Mohmmedaw/dpa/picture alliance

Baada ya ufichuzi mkubwa uliofanywa na mashirika makubwa ya habari kwamba viongozi wapatao 35 wanamiliki makampuni yanazowekeza nje ya nchi zao ili kukwepa kulipa kodi, baadhi ya viongozi hao wanakana kumiliki mali hizo na wengine wakisema hawajawahi kukwepa kodi na wengine wakisema uchunguzi huo hauna msingi wala uthibitisho wowote. 

Soma Zaidi: Nyaraka za Pandora: Wanasiasa wakubwa watajwa kukwepa kulipa kodi

Miongoni mwa wakuu waliojitetea hii leo ni mfalme wa Jordan, Abdullah wa II. Amekanusha kununua jumba la kifahari nje ya nchi, huku akizingatia masharti ya kiusalama yaliyomtaka kutozungumzia mali zinazopindukia dola milioni 100. Amesema mali hizo zilikuwa zikitumika kwa ajili ya shughuli za kiofisi na kwamba, hakukua na fedha ya umma iliyotumika kwa manunuzi na kwa maana hiyo ripoti hiyo amesema, haina maana yoyote kwa kuwa hakuweka wazi kwa sababu ni suala la kiusalama.

Ufichuzi huu wa nyaraka za Pandora umesema mfalme Abdullah alinunua majumba 14 kati ya mwaka 2003 na 2017 kwa kutumia makampuni yaliyosajiliwa kwenye maeneo ambako hawatalipa kodi. Majumba hayo yaliyoko Marekani na Uingereza yana thamani ya zaidi ya dola milioni 106. Taarifa ya kasri la kifalme imesema majumba hayo hutumiwa na wanafamilia wanapotembelea nchini humo, maafisa wa serikali na wa kigeni.

Urusi imesema ripoti hiyo haina msingi wowote.

Mbali na Mfalme Abdullah, ikulu ya Kremlin nchini Urusi imesema hayo ni madai yasiyo na msingi, baada ya washirika wa Rais Vladmir Putin kuhusishwa. Putin anajikuta kwenye kashfa hiyo akihusishwa na jumba la kifahari analomiliki mwanamke anayedaiwa kuzaa nae, anayeishi Monaco.

Wladimir Putin, Präsident Russland | Porträt
Rais Vladmir Putin anahusishwa na jumba la kifahari lililoko Monaco analoishi mwanamke anayedaiwa kuzaa naye. Picha: Sputnik/Vladimir Smirnov via REUTERS

Msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov amesema hakuna mali yoyote iliyofichwa na taarifa hiyo haikuwa wazi na wala haiaminiki.

Pamoja naye ni waziri mkuu wa Jamhuri ya Czech Andrej Babis ambaye pamoja na kusema ripoti hiyo ni uongo mtupu, lakini pia ni chokochoko zinazolenga kumuharibia mbio zake kuelekea uchaguzi wiki ijayo.

"Sina mali yoyote nchini Ufaransa, sina milki yoyote nje ya nchi, nakataa kabisa kwamba kuna utakatishaji wa fedha, kama mtu anavyojaribu kupendekeza, ninakataa." alisema Babis

Huko Afrika Mashariki nchini Kenya, Rais Uhuru Kenyatta aliyehusishwa na ripoti hiyo amesema kupitia taarifa iliyosambazwa na msemaji wa serikali Kanze Dena Mararo kwamba ripoti kama hizi zitasaidia kuongeza uwazi wa kifedha ambao Kenya na ulimwengu wanauhitaji, na kwamba mwenendo wa fedha haramu, mapato ya uhalifu na rushwa hustawi katika mazingira ya usiri na giza.

Familia ya Kenyatta yaguswa kashfa ya Pandora Papers

Kenyatta aliyeko ziarani nchini Marekani amesema atajibu madai dhidi yake atakaporejea nyumbani akitokea zaiarani, Marekani.

Huku viongozi hao wakihangaika kujitenga na kashfa hiyo, Ujerumani kupitia msemaji wake Steffen Seibert imesema ufichuzi wa nyaraka za Pandora uwe kama motisha zaidi wa kupambana na ukwepaji kodi, na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa kukabiliana na tatizo hilo.

Sikiliza Zaidi: 

04.10.2021 Matangazo ya Mchana

Mashirika: AFPE/APE/DPAE