1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waasi wa Yemen kusini wasonga mbele

Oumilkheir Hamidou
29 Januari 2018

Watu wasiopungua 13 wameuwawa na zaidi ya 130 kujeruhiwa kufuatia mapigano kati ya waasi wanaopigania kujitenga eneo la kusini mwa Yemen na vikosi vya serikali katika mji wa bandari wa Aden.

https://p.dw.com/p/2rgpe
Jemen | Bodyguard eines Separatistenführers in Aden
Picha: Reuters/F. Salman

Mapigano katika mji huo wa kusini mwa Yemen, Aden, makao makuu ya serikali  inayotambuliwa kimataifa, yameripuka jana, baada ya kumalizika muda uliowekwa na waasi wanaopigania kujitenga eneo la kusini, kuitaka serikali ijiuzulu. Waasi hao wanasemekana wanaungwa mkono na falme za nchi za kiarabu au emirati, mshirika mkubwa katika muungano unaoongozwa na Saud Arabia dhidi ya waasi wa kishia wa Houthi , wanaopigana vita tangu mwaka 2015 dhidi ya serikali inayotambuliwa kimataifa ya rais Abed Rabbo Mansour Hadi.

Kiongozi wa zamani wa vikosi vya wanajeshi wa Yemen, waziri wa ulinzi Mohammed Ali Al-Miqdashi anasema: "Hakuna tofauti kati ya wahuthi na kundi lolote lile linalofanya uasi dhidi ya serikali halali-hatujali anatokea, kushoto, kulia, kusini au mashariki. Ikiwa haungi mkono serikali halali, basi ni muasi na ataangaliwa kuwa ni adui wa nchi nzima."

Waasi wanaopigania kujitenga Yemen Kusini
Waasi wanaopigania kujitenga Yemen KusiniPicha: Getty Images/AFP/S. Al-Obeidi

Waasi watuma wanajeshi zaidi Aden

Waziri wa ulinzi Al Miqdashi anasema vikosi vya serikali vitapambana na njama yoyote ya kutaka kuigawa nchi hiyo. Waasi hao wanaoungwa mkono na nchi za emirati wametuma vikosi zaidi kutoka mikoa wanayoishikilia ya kusini, Marib na Abyan hadi katika mji mashuhuri wa bandari wa Aden hii leo katika wakati ambapo mapigano yanaendelea. Duru za usalama na za mashirika ya misaada ya kiutu zinasema waasi hao wanayashikilia makao makuu ya serikali.

Shirika la kimataifa la msalaba mwekundu limesema katika ripoti yake kupitia mtandao wa twitter, mapigano yameendelea usiku kucha jana kuamkia leo na silaha nzito nzito zikitumika. Mkuu wa tume ya shirika hilo la kimataifa la Msalaba mwekundu Alexandre Faite lenye makao yake makluu mjini Sanaa mji mkuu wa Yemen anasema mapigano yanayoendelea yamewafanya wafunge ofisi zao mjini Aden na Taiz.

Mandhari ya mji wa bandari wa Yemen-Aden
Mandhari ya mji wa bandari wa Yemen-AdenPicha: Reuters/F. Salman

Vuguvugu la kutaka kujitenga Yemen Kusini

Mzozo ulioripuka jana kati ya waasi wanaopigania kujitenga eneo la kusini na serikali ya rais anaeishi uhamishoni nchini Saud Arabia Abed Rabbo Mansour Hadi unazidisha makali ya mzozo unaoendelea tangu miaka mitatu iliyopita katika nchi hiyo masikini kabisa ya bara arabu. Mzozo huu wa sasa umeanza april mwaka jana baada ya rais Hadi kumuachisha kazi gavana wa jimbo la Aden, Aidarous al Zoubaidi.

Itafaa kusema hapa kwamba Yemen Kusini ilikuwa nchi huru kabla ya kuungana na Yemen kaskazini mwaka 1990 lakini vuguvugu la kujitenga daima lilikuwa na nguvu katika eneo hilo la kusini.

 

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir:AFP/AP/Reuters

Mhariri:Yusuf Saumu