1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel ziarani Hungary

3 Februari 2015

Juhudi za viongozi wa Ugiriki kutaka yajadiliwe upya masharti ya mikopo ,ziara ya kansela Angela Merkel nchini Hungary na azma ya Marekani kuipatia silaha Ukraine ni miongoni mwa mada magazetini.

https://p.dw.com/p/1EUoU
Ureno yapinga kufutwa madeni ya UgirikiPicha: DW/J. Faget

Tuanzie lakini na juhudi za viongozi wepya wa Ugiriki za kutaka masharti ya mikopo yadurusiwe.Gazeti la "Oldenburgische Volkszeitung" linaandika:"Hadi dakika hii,yote yaliyotamkwa na Tsipras,hayaeleweki.Anazungumzia kuhusu kuitishwa mkutano wa Umoja wa ulaya utakaojadili suala la madeni, na pia kuhusu sera za kuhimiza ukuaji wa kiuchumi.Porojo tupu.Madai ya Tsipras ya kutaka madeni yafutwe hayana msingi.Akishindwa kupata fedha,hapo nchi yake itafilisika na hali nchini Ugiriki itamgeukia.Misaada ziada anaweza tu Tsipras kuipata akiregeza kamba.Kwasasa anaonyesha amenasa katika mtego aliyouweka mweyewe.

Werevu wa waziri mkuu wa Hungary

Ziara ya kansela Angela Merkel nchini Hungary nayo pia imemulikwa na wahariri wa magazeti ya humu nchini wanaojiuliza kama imesaidia kumzinduwa waziri mkuu wa nchi hiyo.Gazeti la "Volksstimme" linaandika:"Licha ya kansela Angela Merkel kushinikiza mfumo wa kidemokrasi uheshimiwe,waziri mkuu Viktor Orban wa Hungary anaonyesha kuendelea bila ya kujali na mfumo wa kimabavu wa serikali yake.Kwasababu hata kama Orban anataka kupata faida za Umoja wa ulaya lakini upande wa pili anaikodolea macho Urusi pia.Wiki mbili kutoka sasa rais Vladimir Putin atafika ziarani mjini Budapest-fedha za Urusi zinapangwa kutumiwa kujenga vinu viwili vya nishati ya kinuklea nchini Hungary.Hata kisiasa wanajongeleana.Na hakuna,si kansela na wala si Umoja wa Ulaya mwenye uwezo wa kufanya la ziada badala ya kutoa onyo.Muungano wa Ulaya, unapewa umuhimu mkubwa zaidi hasa wakati huu wa mzozo wa Ukraine.

Kila la kufanywa lifnywe kuepuka vita visienee Ukraine

Mada ya mwisho magazetini inatupeleka Marekani na azma ya nchi hiyo kuipatia silaha serikali ya Ukraine kuweza kukabiliana na waasi wanaopigania kujitenga eneo la mashariki la nchi hiyo."Gazeti la Lausitzer Rundschau linahisi huo sio ufumbuzi". Kutuma silaha za Marekani katika uwanja wa vita nchini Ukraine itamaanisha mwisho wa makubaliano ya kuweka chini silaha.Kwasababu hapo Moscow itaiangalia jumuia ya kujihami ya NATO kuwa ni adui na kujipatia kisingizio cha kutoficha tena vituko vyake.Ndio maana kwa wakati wote ule ambao itaibuka nafasi japo ndogo ya kuendeleza mazungumzo ya kuumaliza mzozo,nchi za magharibi zitafanya la busara kujizuwia na mipango yoyote ya kutuma silaha.La sivyo Urusi itaendelea kuvieneza vita hivyo.Na wakati huo,hakutakuwa na la kufanya."

.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman