1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waislamu wauanza mwezi mtukufu chini ya vizuizi vya corona

Amina Mjahid
13 Aprili 2021

Waislamu wameanza mfungo wa Ramadhan kwa ibada ya pamoja iliyofanywa kwa kuzingatia masharti ya kudhibiti virusi vya corona tofauti na mwaka uliopita kutokana na janga la COVID 19.

https://p.dw.com/p/3rvcx
Indonesien Ramadan - Istiqlal Moschee in Jakarta
Picha: Achmad Ibrahim/AP Photo/picture alliance

Kutoka Indonesia hadi Misri pamoja na waislamu wengi duniani wameanza mfungo wa Ramadhani baada ya viongozi wao wa kidini kuthibitisha kuwa mfungo utaanza siku ya Jumanne huku mfumo wa kuabudu hadharani ukitofautiana nchi hadi nchi.

Msikiti wa Jarkata wa Istiqlal uliokarabatiwa hivi karibuni ambao ni mkubwa katika eneo la Kusini Mashariki mwa Asia jana Jumatatu usiku uliwakaribisha waumini kwa mara ya kwanza baada ya kufungwa kwa zaidi ya mwaka mmoja kutokana na janga la corona.

Akizungumza na shirika la habari la AFP, Mohamad Fathi, Mkazi wa mji mkuu huo wa Indonesia Jarkata  amesema mwaka huu Ramadhan inaonekana kuwa ya furaha kuliko mwaka uliopita wakati watu walipokatazwa kuhudhuria swala maalum ya usiku ya Taraweh. Fathi amesema mwaka huu angalau atahudhuria sala zake msikitini lakini kwa masharti.

soma zaidi: Waislamu waanza mfungo wa mwezi wa Ramadhani

Deutschland Symbolbild Ramadan in der Corona-Pandemie
Mwanamke anayefanya ibada nyumbani kutokana na COVID 19Picha: Dwi Anoraganingrum/Future Image/imago images

Serikali ya taifa hilo lililo na idadi kubwa ya waislamu duniani imeweka masharti magumu. Misikiti ikikubaliwa kuwa na asilimia 50 tu ya waumuni, huku wakitakiwa kuvalia barakoa na kuleta miswala yao au mahala watakaposualia na kufanya ibada zao.

Maeneo mengi pia ya kufungulia mwadhini hadharani yamefungwa na viongozi wa kidini wametoa wito kwa watu kufanya ibada zao nyumbani hasa katika maeneo yaliyo na maambukizi makubwa ya virusi vya corona.

Ibada ya Umrah inafanyika kwa waliopokea chanjo ya COVID 19

Nchini Saudi Arabia kuliko maeneo matakatifu ya kuabudu kwa waumuni wa kiislamu, serikali huko imetangaza mfungo kuanza hii leo huku watu waliopokea chanjo ya COVID 19 wakikubaliwa kufanya ibada ya Umrah.

Nchini Misri mambo hayakuwa magumu vile ikilinganishwa na mwaka uliopita, watu walikubaliwa kuwepo barabarani wakati wanapoanza mfungo wa Ramadhan ambapo waumini wa dini ya kiislamu wanahimizwa kufunga kula na kunywa na kuacha starehe kuanzia jua linapochomoza alfajiri hadi linapozama jioni. 

Baadhi ya mataifa mengine kama Pakistan, Iran na mataifa mengine ya Afrika waumini wa dini hiyo ya kiislamu wataanza kufunga hapo kesho kutokana na tofauti za kalenda ya dini hiyo na muandamo wa mwezi.

Maandalizi ya ramadhani kwa mayatima Dar es Salaam

Kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya corona duniani kumegubika kuanza kwa mwezi mtukufu wa Ramdhani kwa, huku kukiwa na hofu ya kutokea kwa maambukizi zaidi.

Bara la Ulaya lililoathirika vibaya kwa virusi vya corona, limeshuhudia vifo vitokanavyo na virusi hivyo vikipindukia milioni 1 huku mataifa ya Asia yakipambana na makali ya ugonjwa huo ulioathiri kwa kiasi kikubwa uchumi wa dunia.

Chanjo dhidi ya virusi hivyo ndiyo matumaini walionayo watu wengi waliochoshwa na masharti ya kuvidhibiti yakiingia mwaka wa pili. Idadi jumla ya watu waliokufa kutokana na ugonjwa wa COVID 19 inafikia watu milioni tatu huku shirika la afya duniani WHO likisema maambukizi yanakuwa kwa kasi licha ya juhudi nyingi zilizowekwa kuyadhibiti.

Chanzo: afp/ap