1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakenya wateremka tena vituoni kumchagua rais wao

Oumilkheir Hamidou
26 Oktoba 2017

Wapiga kura wa Kenya wanateremka vituoni katika uchaguzi wa marudio wa rais unaosusiwa na muungano wa upande wa upinzani - NASA. Na ripoti zinazungumzia pia kuhusu machafuko katika baadhi ya ngome za upande wa upinzani.

https://p.dw.com/p/2mXMt
Kenia Wahl - Präsident Uhuru Kenyatta
Picha: Reuters/S. Modola

Uchaguzi huo wa marudio umeitishwa baada ya korti kuu kuyakataa matokeo ya uchaguzi wa Agosti nane iliyopita ambapo rais wa sasa Uhuru Kenyatta aliiibuka na ushindi kwa kuyataja kuwa hayakuwa "ya uwazi na wala hayathibishiki."

Kiongozi wa Upinzani Raila Odinga aliyekuwa wa mwanzo kudai uchaguzi uitishwe upya, amesema hatoshiriki kwa kuwa madai yake ya marekebisho ya mfumo wa kupiga kura hayakuitikwa.

Kibera, mojawapo ya mitaa maarufu ya mabanda sawa na Kisumu, mji mkubwa wa magharibi ya Kenya ambako waandamanaji wametia moto mipira ya magari na kuweka vizuwizi majiani, vituo  vinane tu kati ya vituo zaidi ya 450 ndivyo vilivyokuwa vimefunguliwa. Polisi wanasemekana wametumia hewa za kutoa machozi kuwatawanya waandamanaji katika mji wa Migori. Na Huruma, mtaa mwengine wa mabanda jijini Nairobi  wapigakura wachache tu ndio waliojitokeza kutoa sauti zao. Sawa na Mathare wanakoishi wafuasi wa kambi zote mbili, wa NASA na wale wa chama tawala Jubelee, wachache tu ndio wanaoonekana hadi sasa kupiga foleni.

 

Machafuko ya wafuasi wa upande wa upinzani Kisumu
Machafuko ya wafuasi wa upande wa upinzani KisumuPicha: picture-alliance/dpa

Hali mbaya ya hewa na wasi wasi ndio sababu watu wengi hawajajitokeza hadi wakati huu vituoni

 

Mvua kubwa na baridi iliyoanza kupiga tangu masaa machache yaliyopita, vinaonyesha kuwaondoshea shauku wapiga kura. Lakini pia wasi wasi wa kuzuka machafuko huenda umewafanya watu wasiteremke kwa wingi vituoni ikilinganishwa na Agosti nane iliyopita.

Jana kiongozi wa muungano wa upande wa upinzani NASA, Raila Odinga aliwatolea wito wafuasi wake "wasalie majumbani au washiriki katika ibada nje ya vituo vya uchaguzi.

Lakini sio wote walioitika wito wa mwanasiasa huyo mzee wa miaka 72. Katika baadhi ya ngome za upande wa upinzani baadhi ya wafuasi wamezifunga njia kuelekea vituo vya kupiga kura, ambavyo baadhi yao vilikuwa tokea hapo vimefungwa kwa sababu vifaa vya kupigia kura havikuweza kupelekwa na wasimamizi wa uchaguzi wakihofia usalama wao.

 

Maandalizi ya uchaguzi Kenya
Maandalizi ya uchaguzi KenyaPicha: Reuters/T. Mukoya

Wakala za nchi za magharibi zatoa wito wakenya wasikilizane

 

Jana usiku baadhi ya wakala za kibalozi nchini Kenya, ikiwa ni pamoja na zile za marekani na umoja wa Ulaya zimetoa taarifa ya pamoja wakielezea "huzuni kubwa walizo nazo kutokana na visa vya matumizi ya nguvu vinavyotokea nchini humo."Kenya inajikuta katika hatari ya kupoteza sifa ilizojipatia tangu mwaka 2008 ikiwa wakenya hawatokaa pamoja mnamo wakati huu muhimu na kuhifadhi demokrasi na misingi muhimu ya uhuru" wamesema mawakala hao wa nchi za magharibi.

 

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/dpa/AFP

Mhariri: Gakuba, Daniel