1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanajeshi kupunguzwa kwa theluthi moja

24 Agosti 2010

Jeshi la Ujerumani "Bundeswehr" linatazamiwa kufanyiwa mageuzi makubwa kabisa, tangu jeshi hilo lilipoundwa miaka 55 iliyopita.

https://p.dw.com/p/OueM
German Defense Minister Karl-Theodor zu Guttenberg walks past soldiers during a swearing-in ceremony in front of the German Reichstag building, which houses the German parliament, in Berlin, Tuesday, July 20, 2010. Four hundred and twenty soldiers will take their oath later Tuesday to commemorate the 66th anniversary of the failed assassination attempt by Col. Claus Schenk Graf von Stauffenberg on Nazi leader Adolf Hitler on July 20, 1944. (AP Photo/Jens Meyer)
Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani, Karl-Theodor zu Guttenberg.Picha: AP

Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani, Karl-Theodor zu Guttenberg anapaswa kupunguza gharama za jeshi kwa Euro bilioni 8.3 ifikapo mwaka 2014. Wakati huo huo vikosi vyake viandaliwe kwa majukumu yake mapya yaliyoibuka miaka ya hivi karibuni. Jana Jumatatu, aliwasilisha mapendekezo yake kwa wataalamu wa masuala ya ulinzi wa vyama vinavyowakilishwa bungeni mjini Berlin.Waziri huyo ametayarisha mapendekezo matano mbali mbali yatakayosaidia kupunguza gharama za jeshi. Wakati huo huo jeshi litakuwa na vikosi vitakavyoweza kutekeleza majukumu yake bora zaidi na bila ya kuhatarisha usalama wa taifa.

Kwa mujibu wa msemaji wa serikali, Steffen Seibert, Kansela wa Ujerumani Angela Merkel alielezwa kwanza kuhusu mipango hiyo. Amesema Guttenberg binafsi anapendelea zaidi pendekezo moja, lakini Merkel asingependelea kupitisha uamuzi kabla ya majadiliano yatakayofanywa na vyama kuhusu suala hilo. Hata hivyo Merkel anaona uwezekano wa mfumo wa jeshi kufanyiwa mageuzi lakini uamuzi hautopitishwa haraka. Kwa upande mwingine, Guttenberg anataka kuona mageuzi hayo ya jeshi yakiidhinishwa upesi iwezekanavyo. Akieleza mpango anaoupendelea alisema:

Bundeskanzlerin Angela Merkel (CDU) und Regierungssprecher Steffen Seibert, aufgenommen am Montag, 16. August 2010, waehrend der Amtseinfuehrung von Seibert im Bundespresseamt in Berlin. (apn Photo/Berthold Stadler)
Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel(kushoto) na msemaji wa serikali Steffen Seibert.Picha: AP

"Huo ni mfumo utakaopunguza wanajeshi lakini vikosi hivyo vitakuwa bora, vitakuwa na uwezo zaidi wa kutekeleza majukumu yake na wakati huo huo vitaweza kulinda usalama wa ndani ipasavyo."

Lakini vyama vya upinzani bungeni Berlin vina maoni mbali mbali kuhusu mapendekezo hayo ya Guttenberg. Kiongozi wa chama cha kisoshalisti cha SPD, Sigmar Gabriel anaunga mkono pendekezo la kubakia na sheria ya kuwaandikisha raia jeshini, bila ya kuwalazimisha kuhudumia jeshini kwa muda fulani. Lakini chama cha Kijani hakijaridhika na mipango ya mageuzi iliyopendekezwa na Guttenberg hasa kuhusu uandikishaji wa wanajeshi kuambatana na sheria. Mwenyekiti wa kundi la wabunge wa chama cha Kijani mjini Berlin, Renate Künast amesema:

Top candidate Renate Kuenast of the Greens, Buendnis 90/Die Gruenen is seen after the German general elections in Berlin, Sunday Sept. 27, 2009.
Mwenyekiti wa kundi la wabunge wa chama cha Kijani mjini Berlin,Renate Kuenast.Picha: AP

"Pasiwepo uamuzi wa nusu njia...yaani mfumo wa kulazimisha kuhudumia jeshini ubakie katika katiba na wakati huo huo kuwepo mfumo fulani wa kuhudumia jeshini kwa hiyari."

Kwa maoni ya mwanachama huyo wa Kijani, utaratibu wa kulazimisha kuhudumia jeshini uondoshwe kabisa na badala yake kuanzishwe mfumo wa kuhudumia jeshi kwa muda mfupi, kuanzia miezi kumi na mbili hadi ishirini na nne kwa wanawake na wanaume. Künast anaamini kuwa kwa njia hiyo, jeshi litaweza kupunguza kiasi ya nafasi 45,000 za ajira. Lakini uamuzi utapitishwa katika majira ya mapukutiko baada ya kufanywa mikutano ya vyama vya CDU na CSU.

Mwandishi: Kiesel,Heiner/ZPR

Imepitiwa na: Hamidou,Oumilkheir