1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanajeshi wa Uturuki wapatiwa hifadhi Ujerumani

Sekione Kitojo
9 Mei 2017

Vyombo vya Habari vya Ujerumani vimeripoti kuwa wanajeshi kadhaa wa Uturuki pamoja na familia zao wamepatiwa hifadhi ya kisiasa , wakati uhusiano kati ya nchi hizo mbili ukiwa umedhoofika.

https://p.dw.com/p/2cebz
Türkei Anti-Regierungs-Demonstration in Istanbul
Mama akiwa nyuma ya Bendera ya UturukiPicha: Reuters/M. Sezer

Wizara  ya  mambo  ya  ndani  ya  Ujerumani  haikuweza  mara  moja kupatikana  kuzungumzia  suala  hilo, lakini kwa  mujibu wa  gazeti la kila  siku  la  Sueddeutsche Zeitung  pamoja  na  vituo  vya televisheni  vya  taifa  vya  WDR  na  NDR, maafisa wamethibitisha kwamba  Ujerumani  imetoa  ishara zinazoelekeza  kwamba  maombi yao  hifadhi  yatakubaliwa  kwa  raia  hao  wa  Uturuki.

Wanajeshi  hao  pamoja  na  familia  zao  ambao  wanahifadhiwa katika  maeneo  yaliyotayarishwa  na  NATO  nchini  Ujerumani, wamepatiwa  hifadhi  katika  uamuzi wa  awali wa  kuomba  hifadhi. Wanajeshi  hao  wa  Uturuki  waliomba  hifadhi  nchini  Ujerumani baada  ya  kukabiliwa  na  mashitaka  kufuatia  jaribio  la  mapinduzi lililoshindwa  Julai 15, mwaka  2016.

Türkei Präsident Erdogan
Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan Picha: picture-alliance/abaca/O. Ozer

Vyombo vya  habari  vya  Ujerumani  vimesema  kwa  mujibu  wa wizara  ya  mambo  ya  ndani  jumla  ya  maombi 414 yamewasilishwa  na  wanajeshi  hao  wa  Uturuki , wanadiplomasia, majaji  na  maafisa  wengine  wa  serikali  wanaoishi  nchini Ujerumani. Idadi  hiyo  inaripotiwa  kuwajumuisha  pia  wanafamilia wa waombaji hifadhi.

Wizara  ya  mambo  ya  ndani   pia  imeeleza  kwamba  jumla  ya watu 262  miongoni  mwa  wanaoomba  hifadhi ni  maafisa  wa Uturuki wenye  pasi  za  kusafiria  za  kidiplomasia, lakini  haikusema ni  maombi  kiasi  gani  yamekuja  moja  kwa  moja  kutoka  kwa wanajeshi  wa  Uturuki  walioko  katika  vituo vya  NATO.

Hakuna  ishara  juu  ya  kiasi  gani  cha  maombi  yamekubaliwa , ama  maelezo  ya  moja  kwa  moja  kutoka  kwa  maafisa  wa serikali  ambao  wanahusika  moja  kwa  moja  na  kushughulikia maombi  hayo , ofisi  ya  shirikisho  inayohusika  na  wahamiaji  na wakimbizi (Bamf).

Türkei Protest für Pressefreiheit
Maandamano nchini Uturuki dhidi ya kubana uhuru wa kujielezaPicha: picture-alliance/dpa/S. Suna

Maafisa  wa  Uturuki  walianzisha  msako  mkubwa  baada  ya  jaribio la  mapinduzi, ambalo  lilishuhudia  maelfu ya  wale  wanaodaiwa kuwa  wanajeshi  wanaomunga  mkono  imamu  anayeishi uhamishoni  nchini  Marekani Fethullah Gülen  walikamatwa  ama kufutwa  kazi  nchini  Uturuki, ambao  serikali  inawaona  kuwa  ni washirika  wa  njama  za  jaribio  hilo  lililoshindwa  la  mapinduzi.

Kwa  mujibu  wa  ripoti  hizo  za  vyombo  vya  habari , maafisa  wa Bamf walisubiri  matokeo  ya  kura  ya  maoni  yenye  utata kuhusiana  na  mabadiliko ya  katiba  ya  Uturuki  kabla  ya  kuchukua uamuzi  kuhusu  maombi  hayo  ya  wanaotaka   hifadhi  ya  kisiasa.

Deutschland Düsseldorf Stimmabgabe zurm Verfassungsreferendum Türkei
Rais wa Uturuki wakipiga kura katika kura ya maoni kuhusu katiba mpyaPicha: picture-alliance/AA/M. Zeyrek

Maafisa  hao  lakini  wanakana  kwamba  kulikuwa  na  uhusiano  wa aina  yoyote  kuhusiana  na  suala  la  mabadiliko ya  katiba. Matokeo  ya  kura  hiyo  ya  maoni  imempa ushindi  mwembamba rais wa  Uturuki  Recep Tayyip Erdogan  kuwa  na  madaraka  mapya chini  ya  mfumo  wa  uongozi  wa  rais. Wakosoaji  wanahofu kwamba  Erdogan huenda  akatumia  vibaya  mfumo  huo  mpya kukandamiza  zaidi  sauti  za  upinzani.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / English page / afpe

Mhariri : Iddi Ssessanga