1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanamgambo nchini Iraq wauteka mji wa Tikrit

12 Juni 2014

Wanamgambo wa kundi lenye mafungamano na mtandao wa kigaidi wa Al Qaeda nchini Iraq wameuteka mji wa Tikrit, mji wa pili kuudhibiti katika kipindi cha wiki moja na wanaripotiwa kuusogelea mji mkuu Baghdad

https://p.dw.com/p/1CH3v
Picha: picture-alliance/dpa

Wanamgambo wa kundi linalojiita dola ya kiislamu ya Iraq na Sham ISIL hapo jana waliuteka mji wa Tikrit,siku moja tu baada ya kuudhibiti mji wa Mosul na kwa jumla tangu mwaka huu kuanza wameidhibiti miji muhimu ikiwemo Fallujah na Ramadi.

Msemaji wa kundi hilo Abu Mohammed al Adnani ameapa kuendeleza mapambano hadi katika mji mkuu wa nchi hiyo Baghdad na mji wa Karbala unaochukulika kuwa mji mtakatifu miongoni mwa waislamu wa kishia.

Baraza la usalama kukutana kwa dharura

Mashambulizi hayo ya ISIL yamelichochea baraza la usalama la umoja wa Mataifa kutisha mkutano wa dharura hii leo kujadili mzozo huo ambao umezua hofu katika jumuiya ya kimataifa.

Raia wa mji wa Mosul wakitoroka mashambulizi ya ISIL
Raia wa mji wa Mosul wakitoroka mashambulizi ya ISILPicha: Getty Images/Afp//Safin Hamed

Marekani pia imetangaza iko tayari kufanya mashambulizi ya angani dhidi ya ngome za wanamgamabo hao kama miongoni mwa hatua za kijeshi kuisaidia serikali ya waziri mkuu Nouri al Maliki kulidhibiti kundi hilo na kurejesha hali ya kawaida.

Iraq imethibitisha kuwa itairuhusu Marekani kufanya mashambulizi ya angani kaskazini mwa nchi hiyo kukabiliana na ISIL. Matumizi ya ndege za kijeshi zisizotumia marubani nchini Iraq baada ya Marekani kuyaondoa majeshi yake nchini humo mwaka 2011 ni mkondo mpya katika suala la usalama katika kanda hiyo.

Hata hivyo msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni ya Marekani Jen Psaki amesema nchi hiyo haina mipango ya kuyatuma majeshi yake tena nchini Iraq ambako wanajeshi 4,5000 wa Marekani waliuawa vitani.

Umoja wa Mataifa walaani mashambulizi

Katibu mkuu wa umoja wa Mataifa Ban Ki Moon ameihimiza jumuiya ya kimataifa kuinga mkono Iraq na kuonya kuwa ugaidi usipewe nafasi ya kuvuruga juhudi za kulirejesha taifa hilo katika mkondo wa kidemokrasia.

Inakisiwa kiasi cha watu nusu milioni wameyatoroka makaazi yao katika mji wa Mosul.Hapo jana wapiganaji waliuvamia ubalozi mdogo wa Uturuki na kuwateka nyara watu 49 wakiwemo,wanadiplomasia,wafanyakazi wa ubalozi huo,polisi na watoto watatu.

Waziri mkuu wa Iraq Nuri al Maliki
Waziri mkuu wa Iraq Nuri al MalikiPicha: picture-alliance/dpa

Vyombo vya habari Uturuki vimeripoti kuwa waziri mkuu Recep Tayyip Erdogan ameitisha mkutano wa dharura wa kiusalama kujadili tukio hilo la kuvamiwa kwa ubalozi na kutekwa nyara kwa raia wake.

Katika hotuba kwa taifa,al Maliki amesema njama fulani ndiyo ilisababisha kushindwa kwa vikosi vya usalama kukabiliana na wanamgamabo hao na kuwaruhusu kuuteka mji wa Mosul.Waziri huyo mkuu wa Iraq amelitaka bunge la nchi hiyo kutangaza hali ya hatari mjini humo.Bunge hilo linakutana leo kufanya maamuzi.

Iran pia imehitolea kuisaidia Iraq kukabiliana na ISIL. Wakati huo mashirika ya ndege ya Iran yamefutilia mbali safari zote za ndege kutoka Tehran kuelekea Baghdad kwasababu za kiusalama na nchi hiyo imeimarisha usalama katika mipaka yake.

Mwandishi:Caro Robi/Ap/dpa/afp

Mhariri: Josephat Charo