1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanaotaka kujitenga Yemeni wadhibiti mji wa Aden

Sekione Kitojo
11 Agosti 2019

Wapiganaji wanaotaka kujitenga Yemen wamepata udhibiti wa mji wa bandari wa Aden, pamoja na maeneo ya viwanja katika jengo la rais  kutoka majeshi tiifu kwa serikali inayoungwa mkono kimataifa, wamesema maafisa usalama.

https://p.dw.com/p/3Niyw
Jemen Aden Soldaten des Southern Transitional Council (STC)
Picha: picture-alliance/Photoshot/M. Abdo

Wanaotaka  kujitenga  wakiungwa  mkono  na  Umoja  wa  falme za Kiarabu  UAE wamekuwa  wakipigana kama  sehemu  ya  muungano unaoongozwa  na  saudi Arabia  ambao  unaounga  mkono serikali lakini  wameyageuka  majeshi  hayo katika  mapigano katika  mji huo wa  kusini. Idadi ya watu waliofariki  katika  mapigano  ya  siku  nne imepanda  na  kufikia  zaidi  ya  watu 70, ikiwa  ni  pamoja  na  raia, maafisa  hao  wamesema.

Jemen | Separatisten in Aden
Wapiganaji wanaotaka kujitenga wameingia katika mitaa ya mji wa AdenPicha: Getty Images/AFP/S. Al-Obeidi

Matukio  ya  hivi  karibuni  yanaweza  kuvuruga  zaidi  muungano huo  ambao  umekuwa  ukipambana   na  waasi  wa  Kihouthi  ambao ni  washirika  wa  Iran  tangu mwaka  2015 kwa  niaba  ya  serikali ya  rais  Abed Rabbo Mansour Hadi , ambayo  kwa  kiasi kikubwa imekuwa  katika  mji  wa  Aden tu.  Wahouthi  wanadhibiti upande wa kaskazini pamoja  na  mji  mkuu Sanaa.

Kanali Turki al-maliki , msemaji wa muungano  unaoongozwa  na Saudi Arabia, alinukuliwa  jana katika  shirika  la  habari  la  serikali ya  Saudia  akisema kuwa "uongozi  wa  pamoja  wa  muungano unatoa wito wa kusitishwa mara  moja  mapigano katika mji mkuu wa mpito wa Yemen, Aden, na  utatumia  nguvu  za  kijeshi  dhidi  ya wale watakaokiuka hatua  hiyo."

Amesema  muungano  huo  wa  kijeshi  unatoa  wito  kwa  baraza  la mpito  la wanaotaka  kujitenga upande  wa  kusini  pamoja  na majeshi  ya  ukanda  wa  usalama "kurejea  mara  moja  katika maeneo  yao  na  kujiondoa  kutoka  katika  maeneo  yote waliyoyakamata  katika  muda  wa  siku  chache  zilizopita."

Jemen Militärparade in der Provinz Marib
Wanajeshi watiifu kwa rais wa Yemen Abdo rabbo Manosour Hadi wakifanya gwaridePicha: picture alliance/dpa

Mkutano wa  dharura

Maafisa  wa  usalama  mjini  Aden , ambao  wamezungumza kwa masharti  ya  kutotajwa  majina kwasababu  hawana mamlaka  ya kuzungumza  na  vyombo  vya  habari, wamesema  majeshi  ya Saudia yamekuwa  yakilinda  ofisi  ya  Hadi  na  mawaziri  wake katika  jengo  la  makao  ya  rais, lakini  majeshi  ya ulinzi  wa  kanda ya  usalama  yako  nje  ya  jengo  hilo.

Wamesema  kiasi  ya  walinzi 300  wa  jengo  la  rais  waliruhusiwa kuondoka  katika  eneo  hilo , na  waziri  wa  mambo  ya  ndani Ahmed al-Maisari pamoja  na  maafisa  wa  ngazi  ya  juu  wa  kijeshi waliondolewa  na  kupelekwa  nchini  Saudi Arabia  siku ya Jumamosi.

Wanaotaka  kujitenga  pia  wamekamata  kambi  ya  jeshi  katika eneo  la  kati  la  Khormaksar, wamesema.

Saudi Arabia  imezialika pande zinazopigana mjini  Aden kwa  ajili  ya "mkutano  wa  dharura"  nchini  Saudi Arabia , kwa  mujibu wa  shirika la  habari  la  Saudi Arabia.

Yemen Militär Panzer
Wanamgambo watiifu kwa rais Abedrabbo manosur Hadi, wanaofahamika pia kama makati ya umma ya upinzani wakiwa katika vifaruPicha: Getty Images

Wanaotaka  kujitenga  baadaye  walisema  katika  taarifa  fupi wamekubali  kusitisha  mapigano  na  mwaliko  wa  mkutano.

Mapigano  yalizuka siku  ya  Jumatano wakati  majeshi  tiifu kwa baraza  la  mpito  la  eneo  la kusini yalipojaribu  kuingia  katika jengo  la  rais  mjini  Aden baada  ya  waziri  wa  zamani  Hani Bin Braik , naibu  mkuu  wa  kundi  hilo  la  STC, kutoa  wito kwa  serikali ya  Hadi  kupinduliwa.