1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanasayansi walenga mpango mkuu wa mabadiliko ya hali ya hewa

Mohamed Dahman30 Aprili 2007

Wataalamu mashuhuri duniani wa mabadiliko ya hali ya hewa wanakutana mjini Bangkok nchini Thailand kujadili mpango mkuu juu ya kupunguza taathira mbaya za ongezeko la kiwango cha ujoto duniani huku kukiwa na kutofautiana sana juu ya namna ya kutekeleza mpango huo.

https://p.dw.com/p/CB4O
Waandamanaji wakishikilia mabango mbele ya ofisi ya Umoja wa Mataifa mjini Bangkok Jumatatu tarehe 30 April 2007 wakidai serikali ichukue hatua haraka kuleta mageuzi ya nishati kutokana na onyo la janga la mabadiliko ya hali ya hewa.
Waandamanaji wakishikilia mabango mbele ya ofisi ya Umoja wa Mataifa mjini Bangkok Jumatatu tarehe 30 April 2007 wakidai serikali ichukue hatua haraka kuleta mageuzi ya nishati kutokana na onyo la janga la mabadiliko ya hali ya hewa.Picha: AP

Kikao hicho cha tatu cha Jopo la Kiserikali juu ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa kinahuduriwa na takriban wanasanyasi na wataalamu 400 kutoka nchi 120 duniani.

Repoti zilizotolewa mapema mwaka huu na jopo hilo zimeonya kwamba Dunia tayari imepata ujoto na kutabiri taathira mbaya sana ikiwa ni pamoja na ukame,mafuriko,vimbunga vikali na kuongezeka kwa njaa na maradhi.

Repoti ya tatu inayotarajiwa kutolewa mwishoni mwa mkutano huo mjini Bangkok hapo Ijumaa inakusudia kuweka njia za kupunguza utowaji wa gesi zenye kuathiri mazingira na kuzuwiya balaa la hali ya hewa bila ya kuathiri sana uchumi wa dunia.

Chartree Chueyprasit mmojwapo wa maafisa waandamizi wa mazingira nchini Thailand amesema katika ufunguzi wa mkutano huo wakati wa kuchukuwa hatua ni sasa kwamba kuongezeka kwa kiwango cha ujoto duniani kunazidi kuwa agenda moto yenye kuhitaji ushirikiano ulioratibiwa kutoka nchi zote.

Lakini kufikia maafikiano hayo kati ya mataifa mengi mno yalio tafauti na kukubaliana juu ya hatua hasa ya kuchukuwa inategemewa kuwa mada ya mjadala mkali ambapo baadhi ya wajumbe wanatabiri kwamba mkutano huo utatekwa nyara na siasa.
Ni vigumu
sana katika majadiliano ya aina hiyo kujaribu kufikia muafaka na kujaribu kupata ufumbuzi endelevu unaowiana.

Umoja wa Ulaya ambao umeahidi kupunguza utowaji wake wa gesi ya carbon dioxide kwa asilimia 20 kutoka viwango vya miaka ya 1990 kufikia mwaka 2020 yumkini ukakabiliana na Marekani na China ambao ni nchi wachafuzi wakubwa duniani wa hali ya hewa kwa utowaji wao wa carbon dioxide.

Mjumbe wa China Sun Guoshun anataraji mkutano huo utaweza kutowa maoni yenye kuwiana sio tu yale ya nchi zilizoendelea.

Kuna matumaini ya kundosha tafauti zao na kufikia muafaka mwishoni mwa mkutano huo na kwamba hatimae ni tathmini inayowiana ya sayansi ambayo ndiio itakayozingatiwa.

Rasimu ya awali ya muhtasari wa jopo hilo wa kurasa 24 inasema kwamba viongozi wa dunia wana muda mdogo wa kupoteza lakini kwamba zana za kupunguza gesi zenye kuathiri mazingira kwa gharama nafuu tayari zinapatikana.

Nishati inayoweza kutumika upya,umeme unaozalishwa kwa nguvu za nuklea na kupandikiza upya misitu yote yamechangaywa pamoja lakini msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Mazingira UNEP anasema rasimu ya repoti hiyo yumkini yote ikaandikwa upya kufikia mwishoni mwa wiki hii.

Magunduzi ya repoti hiyo ambayo huishia kwa kutowa mapendekezo tu itatumika na serikali na mashirika ya kimataifa kupanga mipango yao wenyewe kwa ajili ya kuzuwiya kuzuka kwa hali mbaya kabisa ya hewa.

Repoti hiyo pia itatimiza dhima muhimu katika mazungumzo ya Itifaki ya Kyoto yatakayofanyika mwezi wa Desemba katika kisiwa cha Bali nchini Indonesia.