1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapalestina kujitangazia uhuru wa nchi yao ?

Abdu Said Mtullya22 Aprili 2011

Rais wa Mamlaka ya ndani ya Palestina Mahmoud Abbas amesisitiza nia ya wapalestina ya kujitangazia uhuru wa nchi yao

https://p.dw.com/p/112Nl


Rais wa Mamlaka ya ndani ya Palestina Mahmoud Abbas amesema halitakuwa jambo la busara kwa Marekani kuwazuia Wapalestina kuwa na nchi yao huru

Abbas aliyasema hayo kwenye mazungumzo na viongozi wa Ufaransa.Wapalestina wanakusudia kuwasilisha kwenye Umoja wa Mataifa mnamo mwezi wa Septemba mpango juu ya kujitangazia nchi yao huru.Abbas aliyasisitiza hayo kwenye mazungumzo yake na viongozi wa Ufaransa. Ametilia maanani kwamba Marekani inaunga mkono mpango wa kuwapo nchi ya Palestina itakayoishi kwa amani pamoja na Israel. Abbas ameeleza kuwa pana ishara nyingi zinazoonyesha kuwa Marekani ipo tayari kuitambua nchi ya wapalestina.

Viongozi wa Palalestina wanafanya bidii ili mpango wa kuwa na nchi yao huru uungwe mkono na wanachama wengi wa Umoja wa Mataifa kwenye baraza Kuu la Umoja huo litakalokutana mwezi wa septemba.

Hadi sasa nchi zaidi ya mia moja zimesema zinaitambua Palestina kuwa nchi.Lakini wanadiplomasia wamesema kuwa Marekani ina mashaka juu ya hatua ya upande mmoja inayochukuliwa na Wapalestina kwa lengo la kuwania dola lao. Wanadiplomasia hao wamesema Marekani inaweza kuzuia kutambuliwa kwa nchi kama hiyo kuwa mwanachama kamili wa Umoja wa Mataifa.

Na waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amesema anataka suluhisho lifikiwe kwa njia ya mazungumzo baina ya pande mbili.

Lakini ndani ya Israel wasomi na wasanii kadhaa wa nchi hiyo wanaliunga mkono lengo la Wapalestina la kujitangazia nchi yao huru.Wasomi na wasanii hao walikutana mjini Tel Aviv mbele ya jengo ambapo miaka 63 iliyopita Waisraeli walitangaza uhuru wa Israel

Mmoja wa wasanii hao Hanna Maron mwenye umri wa miaka 87 alisoma tamko la kuunga mkono nia ya Wapalestina ya kuwa na nchi yao huru.Alisema katika tamko hilo kuwa uhuru wa mataifa mawili ya Israel na Palestina utakaoziimarisha pande zote, ni wajibu wa uadilifu na pia ni msingi wa uhai wa wote. Amesema uhuru huo pia ni msingi wa ujirani mwema.

Hanna Maron ametoa mwito kwa wananchi wote wa Israel, kwa bunge la nchi yake na kwa watu duniani kote, na serikali zao zizitambue nchi zote mbili. Msanii huyo alilisoma tamko hilo lililotiwa saini na wasomi na wasanii wengine 50, wakati ambapo Wapalestina wenyewe wanajitayarisha kuliwasilisha ombi la kutangaza uhuru wa nchi yao kwenye kikao cha Baraza kuu la Umoja wa Mataifa kitakachofanyika mwezi Septemba mwaka huu.

Msanii huyo aliezaliwa nchini Ujerumani alijeruhiwa wakati Wapalestina walipowashambilia abiria waliokuwa wanasubiri kupanda ndege ya Israel kwenye uwanja wa ndege wa Munich mnamo mwaka 1970.

Wasanii hao wamesema katika tamko lao kuwa wanaunga lengo la Wapalestina la kujitangazia uhuru wa nchi yao.

Mwandishi/Verenkotte, Clemens/

Tafsiri Mtullya abdu/

Mhariri/- Josephat Charo