1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WASHINGTON: Maelfu waandamana nchini Marekani kupinga vita.

28 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCX6

Maelfu ya watu wanaopinga vita wameandamana mjini Washington wakitaka majeshi ya Marekani yaondolewe nchini Iraq.

Wanaharakati wa kutetea amani na wabunge kadhaa wanaopinga vita, walijumuika na baadhi ya watu ambao jamaa zao ni askari wa Marekani waliouawa vitani nchini Iraq.

Mcheza-filamu maarufu, Jane Fonda aliyesifika kwa kupinga vita vya Vietnam, alisema haifai kwa wamarekani kuvinyamazia vita vya Iraq.

Maandamano hayo yametokea siku mbili tu baada ya kamati ya bunge la Marekani ya Uhusiano wa Kimataifa kupiga kura dhidi ya mpango wa Rais George W. Bush kuongeza idadi ya wanajeshi elfu ishirini na moja na mia tano nchini Iraq.

Ikulu ya White House imezungumzia maandamano hayo kwa kusema kwamba nia ya mkakati mpya wa Rais George Bush ni kumaliza kabisa tatizo hilo la vita.

Tangu vita hivyo vilipoanza mwaka elfu mbili na tatu, maelfu ya raia wa Iraq na pia askari zaidi ya elfu tatu wa Marekani wameuawa.